BAADA ya mapigano ya Lukaya, eneo la katikati ya Lukaya na Kampala lilikuwa na wapiganaji wengi wa Iddi Amin na Libya waliokuwa wakikimbia. Ndege tatu zilizobeba askari wa Libya waliojeruhiwa ziliondoka mjini Entebbe kwenda Tripoli, Libya.
Wanajeshi wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) waliokuwa wanasonga mbele kuelekea mji wa Kampala walipofika eneo la Buwama walikuta basi la abiria lililokwama njiani na walipochunguza, wakagundua kuwa ‘abiria’ hao ni askari wa Iddi Amin waliokuwa wanakimbia. JWTZ hawakulipua basi hilo, lakini waliwaua askari 20 wa Amin waliojaribu kuwatoroka.
Katika eneo la Mtola Maria, kwa mujibu wa ‘War in Uganda’, askari wa Tanzania walikuta kanisa na shule, wakaona ni heri wapumzike. Ndani ya kanisa hilo mlikuwa na kinanda. Askari mmoja wa JWTZ aliyekuwa amechoka na kuchafuka sana matope alikitumia kinanda hicho kupiga Wimbo wa Taifa, “Mungu Ibariki Afrika.”
Kituo kilichofuata kilikuwa ni Mpigi, kiasi cha kilomita 32 kufika mji wa Kampala. Taarifa za kiintelijesia ziliifikia JWTZ kwamba askari wa Amin waliokuwa wamejiimarisha sana walikuwa wamejichimbia katika eneo hilo.
Kwa kuweka mikakati sawa, Jenerali Msuguri aliamua kuwa brigedi mbili—207 na 208—ziende moja kwa moja Mpigi. Msuguri alipanga Brigedi ya 201 ifagie njia kuelekea upande wa Magharibi kudhibiti barabara na reli inayotoka Kampala kuelekea mji wa Fort Port ulioko Magharibi mwa Uganda.
Brigedi ya 201 ilipoanza kufagia njia, ilikutana na shamba la kahawa karibu na Mityana ambako askari wengine wa Libya walikuwa wameweka kambi yao. Kabla askari wa Libya hawajajua kinachotokea, askari wa JTWZ wakawashambulia kama radi. Ndani ya dakika chache askari zaidi ya 30 wa Libya wakawa wameuawa.
Baada ya hapo askari wa JWTZ wakaendelea kusonga mbele. Lakini wakakabiliwa na changamoto nyingine. Kwa sehemu kubwa ya barabara, askari wa Tanzania walikuwa wakitembea kwenye matope kiasi cha mabuti yao kuzama kabisa na walikuwa wamelowa chapachapa kutokana na mvua iliyokuwa ikinyesha mfululizo.
Kadiri walivyokuwa wakisonga mbele, ndivyo walivyokuwa wakikutana na vikundi vya askari wa Iddi Amin. Sasa kwao ilikuwa ni kuua tu askari wa Amin kadiri walivyokutana nao. Waliendelea pia kuteka vifaru, mizinga midogo na mikubwa, magari mbalimbali ya kijeshi, hususan Land Rover na mabasi ya jeshi, ilimradi walinyakua chochote cha Majeshi ya Amin walichokitia machoni.
Kupitia darubini za kijeshi, JWTZ waliona gari aina ya Mercedes Benz ikiingia Mpigi na baadaye kusimama eneo hilo. Askari wa Tanzania wakajua huyo alikuwa Iddi Amin amefika eneo hilo akiwa katika gari hilo.
Baadaye askari wa Tanzania wakawa na hakika kuwa huyo alikuwa ni Iddi Amin kwa sababu baadaye siku hiyo, Redio Uganda ilitangaza kuwa Rais wa Uganda alikuwa anahutubia mkutano wa hadhara eneo la Mpigi.
Hata baada ya kujua kuwa aliyefika eneo hilo ni Iddi Amin na kwamba wangeweza kumtia mikononi, askari wa Tanzania waliamua wasimfanye chochote. Walimwacha hadi alipomaliza kuhutubia akajiondokea zake.
Makamanda wa JWTZ waliokuwa mstari wa mbele walikubaliana kuwa wasimuue hata kama fursa ya kufanya hivyo ingepatikana.
Sababu ya uamuzi huo ni kwamba ikiwa Amin angeuawa, huenda nafasi yake ingechukuliwa na mtu mwingine na hivyo kuwanyima askari wa Tanzania fursa ya kuishuhudia Kampala ikiangukia mikononi mwa Tanzania.
Hatimaye askari wa Tanzania walipoingia Mpigi, walikuta mji huo mdogo ukiwa tayari umekimbiwa na watu na uporaji ulikuwa wa kiwango cha juu. Askari wa Amin walichukua chochote walichoweza kubeba na kisha kukimbilia Kampala.
Sasa Iddi Amin alikuwa katika hali ngumu kuliko wakati mwingine wowote tangu alipoipindua Serikali ya Dk Milton Obote miaka minane iliyopita.
Mawasiliano ya barabara na reli kutoka Kampala kwenda Fort Port sasa yakawa tayari yameshakatwa. Njia pekee ya kutoka Kampala kwenda Fort Port ikabaki kuwa ni helikopta, lakini marubani wengi wa jeshi la anga la Uganda nao tayari walikuwa wameshakimbia kazini.
Kutoka sehemu zilizoinuka za Mpigi, sasa askari wa Tanzania wangeweza kuishambulia kwa urahisi Entebbe na Kampala.
Jeshi la Uganda sasa lilikuwa limeshachanganyikiwa huku wapiganaji na maofisa wake wakiwa katika hali ya hofu kubwa iliyowasababisha kukimbia ovyo huku na huko.
Kama ni mchezo wa karata, basi Iddi Amin alitumia vibaya karata alizopewa na rafiki yake, Muammar Gaddafi wa Libya.
Rais Nyerere, akizungumzia tishio la Gaddafi la kumuondoa Uganda, alisema“…Pamoja na kwamba (Libya) wanaongeza uzito katika vita, hawawezi kubadilisha msimamo wa Tanzania. Amin atabaki yuleyule mshenzi, muuaji, haaminiki... Ila sasa najua atavimba kichwa zaidi kwa kujua kwamba ana nguvu na nchi tajiri nyuma yake. Na nguvu hiyo sasa imetamkwa rasmi. Si ya kifichoficho tena. Amin atavimba kichwa zaidi.”
Miji mikubwa ya Uganda ambayo sasa ilikuwa imewekwa kwenye shabaha ya kutekwa ilikuwa ni Entebbe na Kampala.
Kwa wakati huo, Iddi Amin alikuwa mjini Kampala akiwahimiza makamanda wa jeshi lake waendelee kupigana vita ambayo wao walijua walielekea kabisa kushindwa.
Ingawa askari wa Libya na wale wa Amin walikuwa wanakimbia vita, bado aliamini tofauti, kwamba atafaulu kuwarudisha nyuma wapiganaji wa Tanzania na kisha kuirudisha ardhi yote ya Uganda kwenye himaya yake.
Sasa askari wa Tanzania walikuwa wameizingira miji ya Kampala na Entebbe, hususan eneo la juu la Mpigi, wakisubiri amri ya kushambulia. Lakini wakiwa wamejiandaa kufanya hivyo, Rais Nyerere alituma neno la kuwaambia wasishambulie kwanza miji hiyo hadi watakapoelekezwa vinginevyo.
Je, kwa nini Mwalimu Nyerere aliwazuia kwanza askari wake kuishambulia na kuiteka miji ya Kampala na Entebbe wakati tayari walikuwa wameshaizingira?

VITA VYA KAGERA: Mwl Nyerere amgomea Muammar Gaddafi

  Aliyekuwa Kiongozi wa Libya, Kanali Gaddafi.

Wakati Tanzania ikiwa imejiandaa kuiteka miji ya Kampala na Entebbe, rafiki mkubwa wa Iddi Amin, Kanali Muammar Gaddafi, alijaribu kumtisha Rais, Julius Nyerere kwa kumwambia ayaondoe majeshi yake nchini Uganda ndani ya saa 24.
Alhamisi ya Machi 29, 1979 Rais Nyerere alilitangazia Taifa kuwa Libya imeitaka Tanzania iyaondoe majeshi yake nchini Uganda katika muda wa saa 24 la sivyo itaingia vitani kikamilifu kumsaidia Amin.
Akizungumza na wazee wa Mkoa wa Dar es Salaam katika Ukumbi wa Diamond Jubilee, Mwalimu Nyerere alisema: “Jumamosi hii iliyopita, Kiongozi wa Libya, Kanali Gaddafi, alimtuma mjumbe wake kuniletea risala. Na risala hiyo inasema hivi, ‘Tangu mgogoro umeanza baina ya Tanzania na Uganda tumejitahidi sana kusuluhisha, lakini sasa baada ya uchunguzi wa muda mrefu, tunaamini Watanzania ndio wachokozi.
“Watanzania ndio waliomvamia Amin, walioivamia Uganda na kwamba vita vinavyoendelea ndani ya Uganda sasa ni vita vya Watanzania wanaoipiga Uganda na wala hakuna Waganda ndani yake…’ Kwa hiyo inasema risala hiyo, ‘naiomba Tanzania itoe majeshi yake nchini Uganda na tunataka majibu katika muda wa saa 24.
“Nilimjibu. Nitaeleza majibu hayo baadaye. Lakini leo nimepata risala nyingine kutoka kwa Kanali Gaddafi. Anasema tuondoe majeshi yetu nchini Uganda katika muda wa saa 24 la sivyo Libya itaingia vitani upande wa Amin.
“Sasa napenda kutoa majibu niliyompelekea Kanali Gaddafi. Nimemwambia balozi wake ampelekee.
“Nimesema, vita hivi vimeanza Oktoba 1978. Vilianzishwa na Amin kwa kuivamia Tanzania na kuchukua eneo lake na kuitangazia dunia kwamba eneo hilo sasa ni sehemu ya Uganda na kwamba kitendo hicho kilikuwa kinatimiza shabaha ambayo Amin alikuwa ametangaza tangu mwaka 1971.
“…Na usuluhishi ulianza wakati uleule. Na sisi tulikuwa tayari kukubali usuluhishi. Na masharti ya usuluhishi tuliyatamka. Tukasema kwanza Afrika ikitambue kitendo hicho kuwa ni kibaya. Ni kitendo cha uvamizi.
“Akemewe huyo. Kusudi kesho na keshokutwa akijaribu kitendo hicho tena ajue atakemewa. Ushahidi wa kumkemea mvamizi uwepo. Pili, aahidi, akane kwamba hataki sehemu yoyote ya Tanzania. Na, tatu, aahidi kulipa fidia kwa uharibifu alioufanya.
“Nitaeleza kwamba haya mawili ya mwisho yangekuwa hayana maana, mtu mwenyewe hana dhamana, lakini lile la kwanza ni la muhimu.
“Nilimweleza balozi kuwa yangetokea tungesikilizana. Tungeafiki. Hayakutokea. Lakini yeye Amin akaendelea kututishia kuwa si tu sehemu aliyoikalia, lakini anajiandaa kukalia sehemu nyingine zaidi za Tanzania.
“Tukaona ushahidi kuwa kweli anajiandaa. Tukaamua kumpiga tena. Tukaamrisha apigwe. Na ndivyo vita hivyo vinaendelea. Na ni vilevile vinaendelea.
“Kwa hiyo nikamwambia balozi amwambie ndugu yetu Gaddafi kuwa kama vita hivi vilikuwa halali wakati vinapigwa katika ardhi ya Tanzania, haviwezi kugeuka na kuwa haramu wakati vinapigwa katika ardhi ya Uganda. Ni vita vilevile.
“Na kwamba vita tunavyopigana sisi ni vita vya usalama wa nchi yetu. Hatukusudii kumtoa Amin. Ni uongo kuwa tunataka kumtoa. Tumeishi naye miaka minane. Tunataka kuwa na hakika kuwa anajua kuwa vita si lele-mama. Kuwa vita si mchezo. Si jambo la kuingia katika nchi ya watu halafu unakwenda unasema uliichukua kwa dakika 25.
“Ajue hivyo. Tunataka ajue kuwa vita si lelemama. Vita si mchezo. Akishajua hilo, madhali tuliishi naye miaka minane, tuko tayari kuishi naye miaka mingine minane.
“…Ndugu Gaddafi alishaniletea ujumbe, na siku hiyo ukarudiwa ujumbe ule. Ukarudiwa siku ya Jumamosi, kwamba tumwamini Gaddafi. Kwamba yeye anachukua dhamana kuwa Uganda haitaishambulia tena Tanzania. Dhamana hiyo anachukua Gaddafi.
“Nilimwambia ndugu balozi amweleze ndugu Gaddafi ugumu wetu sisi kukubali dhamana hiyo. Nilieleza sababu mbili.
“Sababu ya kwanza, Amin haaminiki. Nikamwambia (balozi) amuulize ndugu Gaddafi yeye anamwamini? Sema mimi namuuliza yeye (Gaddafi) anamwamini Amin? Anaweza kuchukua Msahafu akasema kwa jina la Allah namwamini Amin? Anaweza?
“Hakuna mtu mwenye akili anaweza kumwamini Amin. Yeye Gaddafi anamwamini? Kwa nini ananiomba mimi nimwamini? Kesho na keshokutwa atamgeuka huyo. Urafiki uliopo baina ya Uganda na Libya kesho utageuka kuwa uhasama.
“Nitamuuliza nani kuhusu usalama wa nchi yangu? Nitamwendea nani kumuuliza wakati huo Amin amekwishamgeuka Gaddafi?
“Nikamwambia balozi, ndugu balozi, mimi nimefurahi sana tangu mwanzo wakati nilipokuwa naupokea ujumbe wa Libya kujaribu kusuluhisha ugomvi baina yetu na Uganda, lakini yalikuwa yanatokea maneno kuwa mpo ndani ya Uganda mnapigana bega kwa bega na Iddi.
“Sisi tumekataa kutangaza habari hii. Tumekataa kuipokea rasmi na kuitangaza. Kwa nini? Kusudi muendelee na shughuli za usuluhishi…
“Pili, huyo Amin ni mkorofi huyo. Sitaki amani naye. Tunataka ajifunze kuwa vita si lele-mama. Akishajifunza tutakuwa na amani baina ya Tanzania na Uganda. Lakini hawezi kujifunza ikiwa anajua kwamba mali ya Libya iko nyuma yake.
“Hayo ni majibu kwa ufupi niliyompelekea ndugu yangu Gaddafi. Na leo amerudisha ya kwake. Amesema tutoe majeshi yetu Uganda, na kama hatukufanya hivyo nchi yake itatoa msaada kwa Uganda.
“Lakini wakiamua kuwa wanamsaidia Amin, pamoja na kwamba wanaongeza uzito katika vita, hawawezi kubadilisha msimamo wa Tanzania. Amin atabaki yuleyule mshenzi, muuaji, haaminiki.
“Ila sasa najua atavimba kichwa zaidi kwa kujua kwamba ana nguvu na nchi tajiri nyuma yake. Na nguvu hiyo sasa imetamkwa rasmi.
“Kwa hiyo hatari kwetu itakuwa ni kubwa zaidi, si inakuwa ndogo. Na kwa hiyo tutajifunza zaidi kumkabili. Lakini tunamkabili Amin. Nataka ndugu zangu wa Libya wajue hivyo. Hatuna ugomvi na Libya. Tunapigana na Amin. Hatupigani na Libya.
“Lakini usalama wa Tanzania ni dhamana ya Watanzania. Utalindwa na Watanzania. Siwezi kumwomba mtu mwingine nimkabidhi usalama wa nchi yangu. Nitaendelea kupambana na wote wanaohujumu usalama huo….
Itaendelea