SIKU nne baada ya Muammar Gaddafi kumwambia Rais Nyerere aondoe majeshi yake nchini Uganda ndani ya saa 24 la sivyo Libya itaingia vitani moja kwa moja kumsaidia Iddi Amin, ndege ya kijeshi ya Libya aina ya Tupolev Tu-22 ilipaa kutoka Uwanja wa Jeshi wa Nakasongola kwenda kupiga mabomu Tanzania.
Kwa mujibu wa kitabu cha War in Uganda: The Legacy of Iddi Amin, ndege hiyo ilikuwa ikiruka futi chache tu juu ya Ziwa Victoria kukwepa kuonekana kwenye rada. Nia yake ilikuwa ni kupiga mabomu matanki ya kuhifadhia mafuta yaliyopo Mwanza. Lakini rubani aliwahi kudondosha mabomu hayo ambayo yalianguka kwenye Kisiwa cha Saanane kilichopo ndani ya Ziwa Victoria.
Jarida la Summary of World Broadcasts: Non-Arab Africa liliripoti kwamba “Ndege ya Libya ya ‘Tupolev-22’ iliyotumwa (na Libya) kwenda Uganda kumsaidia Iddi Amin, jana saa 12:25 jioni ilirusha mabomu matano katika mji wa Mwanza eneo la Butimba katika Kisiwa cha Saanane.”
Jarida la Daily Report: People’s Republic of China liliandika kuwa, “Katika tukio hilo mtu mmoja alipata majeraha kichwani na mikononi ... vyanzo vya habari za kijeshi vinasema mabomu hayo yalikusudiwa kupigwa kwenye matanki ya hifadhi ya mafuta mjini Mwanza.”
Taarifa nyingine zilisema majeruhi pekee katika shambulio hilo alikuwa mfanyakazi wa hifadhi ya kisiwa hicho. Swala sita waliuawa pamoja na ndege kadhaa.
Tanzania ilijibu mapigo siku mbili baadaye. Ndege za Tanzania zilipaa kutoka Mwanza na kwenda kupiga mabomu katika miji ya Kampala, Jinja na Tororo. Kwa mujibu wa Xinhua Weekly, Aprili 2, 1979 ndege za Jeshi la Tanzania ziliupiga mabomu mji wa Jinja ambao ni wa pili kwa ukubwa na mji wa viwanda nchini Uganda, kiasi cha kilomita 70 Kaskazini mwa mji mkuu wa Kampala.
Katika mji wa Jinja, rubani wa Tanzania alifanikiwa kuipiga bomu Benki ya Maendeleo ya Libya-Uganda. Amin alikuwa mjini Jinja wakati mji huo ukishambuliwa. Hata hivyo, shambulizi hilo halikudumu kwa zaidi ya sekunde 10.
Kitendo cha ndege ya Tanzania kufanikiwa kulenga shabaha na kuitwanga Benki ya Maendeleo ya Uganda-Libya kiliwashangaza sana askari wa Amin kiasi cha kuwafanya waamini kuwa Tanzania ilikuwa na silaha kali.
Ndege zote za Tanzania zilirejea salama baada ya kufanya mashambulizi na siku mbili baadaye zikafanya shambulio jingine ndani ya Uganda. Safari hii uwanja wa ndege wa Entebbe ulishambuliwa, lengo likiwa ni kuuharibu ili ndege za Libya zisiweze kutua.
Kutoka kwenye miinuko ya Mpigi, Watanzania waliweza kuona mji wa Kampala kwa upande wa Kaskazini na Entebbe kwa upande wa Mashariki. Ndege za Libya zilionekana zikitua na kupaa na idadi kubwa ya askari wa Amin na wale wa Libya walikuwa Entebbe.
JWTZ iliona kuwa ikiwa wangeutwaa mji wa Kampala kabla ya ule wa Entebbe, askari wa Tanzania wangekabiliwa na jeshi kubwa la adui nyuma yao. Jenerali Msuguri aliamua waende kwanza Entebbe na kazi hiyo akakabidhiwa Brigedia Mwita Marwa wa Brigedi ya 208.
Kwa siku tatu mfululizo yalikuwa yakirushwa mabomu mawili au matatu kuelekea Entebbe. Wakati bomu moja lilipodondoka eneo la maegesho ya magari la Ikulu ya Entebbe, Amin akawa na uhakika kuwa wanajeshi wa Tanzania walikuwa wamemkaribia. Mara moja akatoka ndani ya Ikulu, akarukia kwenye helikopta iliyokuwa nje na kupaa kuelekea Kampala.
Jumanne ya Aprili 3, 1979 matangazo ya Redio Uganda yakasema, “Amin yuko mapumzikoni na ni mwenye furaha mjini Jinja.” Taarifa ikaendelea kusema, “Rais wa maisha wa Uganda amepuuza taarifa kwamba alikimbia na amewahakikishia wananchi wa Uganda kwamba yeye kama mshindi wa himaya ya Uingereza amejiandaa kufa akiitetea nchi yake.”
Ilipofika Aprili 6 mashambulizi ya Tanzania katika mji wa Entebbe yakaongezeka. Asubuhi iliyofuata Brigedi ya 208 ilikuwa inasonga mbele. Miongoni mwa mashambulizi waliyofanya siku hiyo ni kulipua gari la jeshi aina ya Land Rover lililokuwa na askari wanane wa Libya wakielekea Mpigi.
Siku hiyo ndege ya mizigo ya Libya, C-130, ikatua uwanja wa Entebbe saa nne asubuhi kujaribu kuwaokoa askari wa Libya walionasa. Askari 30 wa Libya walikazana kuingia ndani ya ndege hiyo kabla haijageuka na kuanza kuondoka. Lakini askari wa Tanzania walikuwa wameshalikaribia eneo hilo na kuilipua. Ndege hiyo ilishika moto ikawateketeza askari wote wa Libya waliokuwa ndani yake.
Mashambulizi kutoka kwa askari wa Tanzania yalipoongezeka, askari wa Libya waliobaki Entebbe walizidi kuchanganyikiwa. Waliingiwa na wazo la kukimbilia Kampala lakini hawakujua njia watakayoifuata kufika huko.
Entebbe ilipozingirwa vya kutosha, askari wa Libya waliobaki nao waliamua kutafuta njia ya kukimbilia Kampala. Malori kadhaa yaliyowabeba askari wa Libya yakisindikizwa na magari mawili ya deraya yalianza safari kuelekea Kampala.
Umbali wa kilomita nane kutoka Entebbe, Luteni Kanali Salim Hassan Boma aliwasubiri. Aliwagawa wapiganaji wake wakae pande mbili za barabara.
Msafara uliowabeba askari wa Libya ulipofika eneo walikojificha askari wa JWTZ, askari wa Tanzania walikaa kimya na bila kujigusa. Makamanda wa Libya walisemezana kwa muda mfupi, kisha askari waliokuwa kwenye magari hayo wakaanza kumimina risasi pande zote mbili za barabara.
Hazikuwagusa askari wa Tanzania. Lakini wakiwa na wasiwasi bado waliruhusu gari moja likatangulia. Walipoona hakuna kinachoendelea, makamanda wa askari wa Libya wakaruhusu magari mengine yaliyojaa askari wao yapite.
Ndipo Luteni Kanali Salim Hassan Boma akatoa amri ya kufanya shambulio. Magari yote ya kivita ya Libya yakashambuliwa na kuteketea kwa moto hata kabla hawajaweza kujibu shambulizi lolote.
Harufu ya kuungua kwa nyama ikatawala eneo hilo. Ndani ya dakika 10 askari wote 65 wa Libya wakawa wamekufa.

VITA YA KAGERA; Majeshi ya Libya yaelemewa na JWTZ nchini Uganda




Kiongozi wa Libya, Muammar Gaddafi hakujua uwezo wa kijeshi iliokuwa nayo Tanzania. Askari wake walipata tabu kubwa walipokuwa Uganda.
Jarida la Africa Research Bulletin la Aprili 1—30, 1979 linasema katika mapigano ya siku mbili ya Entebbe, kiasi cha askari 400 wa Libya waliuawa na wengine zaidi ya 40 walichukuliwa mateka.
“Tanzania pia ilikamata kiasi kikubwa cha silaha nzito za Libya na ndege kadhaa za kijeshi za Jeshi la Uganda,” linasema.
Kitabu cha War in Uganda kinasema mradi wa Muammar Gaddafi nchini Uganda uligeuka kuwa ni maafa kwa askari wake.
Makumi ya askari wa Libya waliojeruhiwa walipelekwa katika Hospitali ya Mulago mjini Kampala na baadaye waliondolewa nchini humo wakitokea kwenye Uwanja wa Ndege wa Nakasongola. Silaha kali za kivita zikiwamo zile za kisasa zikaangukia mikononi mwa askari wa JWTZ.
Askari wapatao 60 wa Libya waliotekwa na askari wa JWTZ, kwa mujibu wa kitabu cha Idi Amin Speaks: An Annotated Selection of His Speeches, walipelekwa Tanzania.
Hata hivyo waliachiwa baada ya miezi mitatu na waliobakia waliachiwa baada ya miezi tisa.
Kitabu cha An Encyclopedic Dictionary of Conflict and Conflict Resolution, 1945-1996 cha John E. Jessup katika ukurasa wake wa 769 kinasema, “Mei 15, 1979, Libya iliilipa Tanzania Dola milioni 40 ili iwaachie mateka wa kivita wa waliokamatwa wakati wa mapigano nchini Uganda.”
Lakini kitabu cha War in Uganda: The Legacy of Iddi Amin katika ukurasa wake wa 122 kimeandika: “Hadithi za kwamba Nyerere aliwauza mateka kwa Gaddafi hazina ushahidi wowote. Gaddafi hakuonekana kama anajali ikiwa mateka watarudi nyumbani au hawatarudi. Nyerere aliahidi ‘Libya itawapata mateka wote. Hatutawauza Hatutafanya biashara ya kuuza wanadamu kwa ajili ya fedha. Sisi ni maskini sana. Tunajali sana heshima ya utu.”
Hata baada ya kuonekana dhahiri kuwa Gaddafi hakuweza kumuokoa Iddi Amin, bado Amin alizililia nchi za Kiarabu akitaka zimsaidie kupambana na Tanzania. Katika matangazo fulani ya redio alilalama kuwa, “Tanzania na rafiki zake Wayahudi” wanapambana na Serikali ya Uganda.
Akasema: “Huu ni wakati ambao nchi za Kiarabu zinapaswa kuisiadia Uganda kifedha na kwa mali.” Lakini Nyerere, kwa upande mwingine, alijitahidi kuhakikisha kuwa dunia haitaona kuwa haya ni mapambano ya Waafrika dhidi ya Waarabu.
Hadi kufika jioni, kikosi cha Luteni Kanali Salim Hassan Boma kikawa kimeiteka Entebbe. Askari wa Iddi Amin walikuwa wamekwishakimbia wakiwaacha wenzao wa Libya wakipata tabu.
Asubuhi ya Jumapili ya Aprili 8, 1979 askari wa Tanzania walianza kuvinjari katika mji wa Entebbe. Walipofika katika kanisa moja walikuta kiasi cha askari 200 wa jeshi la anga la Iddi Amin wamejikunyata, wakiwa wamevalia nguo za kiraia, wakiwa wamejiandaa kujisalimisha.
Maduka kwenye Uwanja wa Ndege wa Entebbe, yalikuwa yameshaporwa na askari wa Iddi Amin wakati wakikimbia. Kulikuwa na ndege tisa za kivita aina ya MiG-21 ambazo kwa mujibu wa kitabu cha Three Thousand Nights of Terror, askari wa Tanzania walidai kuwa hiyo ni zawadi ya vita. Ndege hizo zilichukuliwa na kupelekwa Tanzania. Lakini wakati zikiwa zinatua, moja ilianguka na kumuua rubani wake.
“Watanzania sasa walikuwa wamedhibiti vita na Ikulu ya Entebbe ilikuwa imeangukia mikononi mwao... Walikuta Ikulu ikiwa imejaa silaha na bidhaa nyingi kama redio, pombe, televisheni,” kimeaendika kitabu cha Three Thousand Nights of Terror.
Sasa askari wa Tanzania walikuwa wanavinjari ndani ya Ikulu ya Entebbe. Meja Jenerali David Msuguri aliwasili Ikulu ya Entebbe saa 3:30 asubuhi.
Mpango wa mwisho wa kuivamiana na kuiteka Kampala ulifanyika kwenye chumba cha chakula cha Ikulu ya Entebbe. Batalioni ya 19 ya Brigedi ya 208 iliyokuwa chini ya Kanali Benjamin Msuya ikapewa jukumu la kuiteka Kampala ambayo sasa ilikuwa umbali wa kama kilomita 35.
Sasa huu ulikuwa ni mpango wa jeshi la nchi moja kuteka makao makuu ya nchi nyingine. Ni historia ya kipekee sana katika Bara la Afrika. Tangu mwanzo wa vita, hakuna askari hata mmoja chini ya Msuya ambaye alikuwa amepoteza maisha kwenye mapigano, na sasa alikuwa amenuia kuiteka Kampala bila kumpoteza askari wake hata mmoja.
Brigedi za 201, 207 na 208 zilijipanga kwa kazi hii muhimu. Wakati mipango ya kuiteka Kampala ikifanyika katika Ikulu ya Entebbe, Idi Amin naye alikuwa mjini Kampala na maofisa wa jeshi lake wakipanga namna ya kuulinda mji huo.
Mapambano makali kati ya askari wa Amin na wale wa Tanzania yalifuata. Hali ya hewa ilikuwa mbaya na mvua ilikuwa ikinyesha bila kukoma. Ingawa mvua ilikuwa inanyesha na askari wa JWTZ wakiwa wamelowa chapachapa, ari yao ilionekana kuwa juu sana.
Baada ya tabu yote ya mapambano ya usiku kucha kuelekea Kampala, asubuhi Msuya na kikosi chake walifika mahali wakafungua redio kusikiliza sauti ya Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) wakasikia taarifa kutoka Nairobi kwamba waandishi wanne wa habari, raia wawili wa Sweden na wawili wa Ujerumani Magharibi, wanaaminika kuwa wameuawa na askari wa Iddi Amin walipokuwa wakijaribu kuvuka Ziwa Victoria kwa mashua wakitokea Kenya kwenda kuandika habari za vita nchini Uganda.
Baadaye ilijulikana kuwa waandishi hao ni Arne Lemberg wa gazeti la Sweden liitwalo Expressen, Karl Bergman wa gazeti jingine la Sweden linaloitwa Svenska Bagvladet, Hans Bolinger ambaye ni mpigapicha wa shirika la habari la Gamm na Wolfgang Steins wa majarida ya Stern na Geo.
Waandishi hawa waliuawa na askari wa Amin kwa kupigwa risasi. Walikodi mashua ndogo kutoka Bandari ya Kisumu ambayo waliitumia kuvuka ziwa, lakini walipofika upande wa Uganda wakajikuta wameangukia kwenye mikono ya askari wa Amin.
ITAENDELEA