BAADA ya kuviteka vilima vya Kikanda, Nsambya na Simba, sasa kazi iliyofuata ni kuteka miji ya Masaka na Mbarara. Vikosi vilivyoelekea Masaka havikupata tabu kama vile vilivyoelekea Mbarara. Brigedia Silas Mayunga aliyekuwa akiongoza Brigedi ya 206 ndiye aliyekutana na hali ngumu zaidi.
Kiasi cha kilomita 45 kutoka mpaka wa Tanzania, karibu na mji wa Gayaza vifaru viwili vya Tanzania vya kikosi cha Luteni Nshimani vilipigwa kombora na majeshi ya Idi Amin.
Kwa jinsi Nshimani alivyokasirika, alianza kuwakimbilia maadui waliorusha makombora hayo. Kitabu cha War in Uganda kinasema alipokuwa akiwafukuza kwenye barabara ya kuelekea ufukweni mwa Ziwa Nakivale, Luteni Nshimani aligutuka kuwa alikuwa akielekea kwenye hatari kubwa.
Karibu na kona mmoja ya barabara hiyo alikutana na mzee mmoja mwanamume aliyekuwa akipita eneo hilo. Alimsimamisha na kumuuliza kama ameyaona majeshi ya Amin maeneo hayo. Mzee alimjibu kwamba wote wameshakimbia.
Wakati Nshimani alipogeuka na kuelekea kwenye kona ya barabara hiyo, mtikisiko mkubwa wa milio ya risasi za bunduki za SMG ulitikisa dunia katika eneo hilo. Risasi hizo zilikuwa zikipigwa kutoka pande tatu.
Watanzania walikuwa wameingia kwenye mtego mbaya kuliko wowote katika vita yote ya Tanzania dhidi ya Uganda. Milio ya risasi ilidumu kwa muda fulani, na ilipotulia hatimaye, tayari Watanzania 25 walikuwa wameshapoteza maisha. Haya yalikuwa ni mauaji makubwa zaidi kwa wanajeshi wa Tanzania kuliko wakati mwingine wowote wa kipindi chote cha vita ile.
Shambulio hili lililofanywa na askari wa Idi Amin lilikuwa ni mojawapo ya yale machache waliyofanya kwa umakini mkubwa kipindi chote cha vita.
Shambulio la Ziwa Nakivale likawatia hasira majeshi ya Tanzania, lakini hawakuvunjika moyo. Wakasonga taratibu kuelekea Masaka upande wa mashariki na Mbarara upande wa magharibi. Katika njia nzima kulikuwa na mapigano karibu katika kila kitongoji—mengine madogo na mengine makubwa.
Maeneo ambayo kulikuwa na mapigano makubwa ni pamoja na miji ya Kyotera, Kalisizo, Bukeri, Sanga, Miakitele na baadhi ya maeneo mengine. Wakati wote huu kusonga mbele kulifanyika kwa tahadhari kubwa kuliko ilivyokuwa kabla ya shambulio la Nakivale.
Wanajeshi wa Jeshi la Amin wakawa wanakimbia ovyo na kufyatua risasi ovyo. Wakihofia mizinga ya Tanzania, askari wa Amin walianza kujificha kwenye miji kwa imani kuwa Tanzania ingesita kupiga mabomu maeneo ya raia na hata kama wangepiga mabomu hayo basi raia wa Uganda wangekasirishwa sana na wanajeshi wa Tanzania na hivyo kushirikiana na askari wa Amin.
Lakini hali ilikuwa kinyume. Raia walikuwa tayari wameshaikimbia miji hiyo hata kabla askari wa Amin hawajafika wala wale wa Tanzania. Kutokana na sababu hiyo, wanajeshi wa Tanzania hawakuwa na hofu ya kutumia mizinga yake kushambulia miji hiyo kwa sababu hawakuwa na hofu ya kuwapo kwa raia katika maeneo hayo.
Vikosi vilivyoelekea Masaka havikupata tabu kama vile vilivyoelekea Mbarara. Brigedia Silasi Mayunga aliyekuwa akiongoza Brigedi ya 206 ndiye aliyekutana na hali hiyo.
Kwa mujibu wa kitabu cha War in Uganda: The Legacy of Idi Amin (uk. 82), wapiganaji wa Tanzania walipofika umbali wa kilometa kama 30 kusini mwa mji wa Masaka walikutana na kijana wa Kitanzana ambaye aliwaambia alitekwa na majeshi ya Idi Amin na kupelekwa Uganda sasa alifanikiwa kutoroka na alikuwa njiani kurudi nyumbani. Walipomhoji zaidi aliwaambia wanajeshi hao kuwa ameacha zaidi ya raia 2,000 wa Tanzania katika kambi ya mateso ya Kalisizo.
Lakini walipofika Kalisizo hawakukuta hata raia mmoja wa Tanzania aliyekuwa ameshikiliwa na, badala yake, waliwakuta askari, wapata 600, wa Amin wakisubiri kushambulia. Huenda tayari walikuwa wameachiwa baada ya kupata habari kuwa majeshi ya Tanzania yanakaribia.
Askari wa Amin waliokuwa wakiwasubiri askari wa Tanzania ili wawashambulie, walianza kufanya hivyo. Lakini walipopigwa mzinga wakajikuta wameyeyuka kama samli kwenye kikaango. JWTZ haikuishia hapo.
Ikaendelea kushambulia zaidi kutokea pande tatu. Askari wa Amin wakachanganyikiwa zaidi. Walipoona hali kwao inazidi kuwa ngumu, waliobahatika kukimbia walianza kukimbia ovyo kuelekea Masaka. Zaidi ya askari 200 wa Amin waliuawa siku hiyo katika shambulio hilo moja la Kalisizo.
Walionusurika kuuawa na wakabahatika kukimbia, walikuwa wakipiga mayowe njia nzima kuelekea Masaka. Askari wa Amin ambao hawakuwa eneo la tukio, lakini wakawaona wenzao wakikimbia kwa hofu huku wakipiga mayowe, nao wakajiunga nao na kuanza kukimbia ovyo. Askari wengine waliopata habari za yaliyotukia walivunjika mioyo na wakapoteza hamu ya kuendelea na vita.
Baada ya ushindi wa Kalisizo, Jeshi la Tanzania walikuwa na nafasi nzuri zaidi za kusonga mbele kuelekea Masaka, lakini badala yake walitulia wakaanza kujipanga.
Usiku wa kuamkia Jumamosi ya Febriari 24, 1979, mji wa Masaka ukawa umezingirwa na JWTZ kwa pande tatu na, baada ya muda mfupi, brigedi za 201 na 208 zikaanza mashambulizi. Sehemu ya kwanza kushambuliwa ilikuwa ni kambi ya jeshi ya Kikosi cha Suicide kilichoachwa peke yake kulinda mji wa Masaka. Vikosi vingine vilikuwa vimetoweka kuelekea Lukaya. Walipoelemewa, kikosi cha Suicide nacho kikatoweka, kikakimbilia Villa Maria.
JWTZ walikuwa na amri ya kuiteketeza Masaka. Mji uliteketezwa. Ilipofika jioni ya Jumamosi ya Februari 24, mji wa Masaka ukawa tayari umeharibiwa vibaya, na sasa majeshi ya Tanzania yakaridhika kwamba Idi Amin ameanza kulipa gharama za kuteka ardhi ya Tanzania. Awamu ya pili ya vita ikawa imemalizika. Sasa ikaingia awamu ya tatu. Nini kilifuata baada ya Masaka kutekwa?
Wanajeshi wa Tanzania wakiwa katika uwanja wa

Hapo ndipo walipokuja kuingizwa akina Yoweri Kaguta Museveni, ambaye alipewa eneo la Mbarara ambako angewafundisha wapiganaji wake na Paulo Muwanga akapelekwa Masaka. Ingawa Muwanga ni wa kabila la Baganda kama wakazi wa Masaka, alionekana zaidi kuwa ni mtu wa Dk Milton Obote. Baada ya muda mfupi Museveni alifanikiwa kupata wapiganaji kiasi cha 2,000 kutoka Mbarara.
Wakati haya yakifanyika, JWTZ nayo ilikuwa inajipanga upya kutokana na hali ilivyokwenda. Ingawa tayari walikwishateka miji ya Masaka na Mbarara, Idi Amin bado alikuwa madarakani na alikuwa mjini Kampala. JWTZ ikaanza safari ya kwenda Kampala aliko Amin.
Brigedi mbili za Minziro na ya 206 zikaungana kuunda kikosi kazi. Wakati huu ndipo Silas Mayunga alipopandishwa cheo kutoka brigedia na kuwa meja jenerali, kisha akakabidhiwa kikosi kazi hicho. Brigedia Roland Makunda, ambaye alikuwa mkuu wa jeshi dogo la maji alikabidhiwa kusimamia Brigedi ya 206, na Brigedia Ahmed Kitete akakabidhiwa Brigedi ya Minziro.
Baadaye kikosi kKazi kikagundua kuwa Kikosi cha Simba ambacho walikishambulia hawakukiteketeza chote. Baada ya kuukimbia mji wa Mbarara kikosi hicho pamoja na kingine kutoka Kambi ya Mountains of the Moon, walikuwa wamekimbilia Kaskazini mwa mji huo kujiimarisha.
Walishtukiwa baada ya kuanza kuwarushia mabomu wanajeshi wa Tanzania. Lakini JWTZ ilipojibu mapigo, walitoweka.
Jumatatu ya Machi 19, 1979 Redio Uganda iliripoti kuwa Idi Amin aliwatembelea wanajeshi wake “...walioko mstari wa mbele eneo la Mbarara...” na kujadiliana “mambo mengi” na makamanda wa vikosi vya Simba na Chui (Tiger) na kwamba walipanga “mikakati mipya ya kuwang’oa kabisa maadui kutoka ardhi ya Uganda.”
Lakini baadaye ilibainika kwamba redio hiyo ilitangaza uongo. Jambo hilo halikutokea. Lakini angalau hicho kikosi cha Simba kiliendelea kupigana huku kikikimbia. Divisheni ya 20 ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania, ambayo ilikuwa inaelekea Uganda, ikakumbana na tatizo jingine la miundombinu wakati kinakaribia eneo la Lukaya, kiasi cha kilomita 40 Kaskazini mwa mji wa Masaka.
Barabara yenye umbali wa kiasi cha kilomita 20 ilikuwa imeharibika vibaya. Kutokana na mvua iliyonyesha barabara hiyo ilijaa madimbwi makubwa ya maji na matope. Hakuna gari lolote lililoweza kupita barabara hiyo, mjia pekee ya kufika huko na kwa kutumia barabara hiyo.
Jijini Dar es Salaam bado Nyerere alikuwa anakuna kichwa. Aiteke Kampala na kumkamata Idi Amin halafu avumilie masuto ya jumuiya ya kimataifa? Au aepuke masuto hayo lakini arudishe majeshi yake nyuma na amwache Idi Amin akiendelea kutawala Uganda?
Idi Amin alijua mpango wa Tanzania wa kuiteka Kampala. Ilisemekana kuwa baadhi ya wanamkakati wake wa kivita walimshauri kuwa ili Kampala isitekwe [kwa urahisi] kama Masaka na Mbarara basi walipaswa kuharibu maeneo fulani ya barabara eneo fulani Kaskazini mwa Lukaya ili kuvunja mawasiliano ya barabara.
Waliambiana kuwa kwa kufanya hivyo kungeyachelewesha zaidi majeshi ya Tanzania kufika Kampala na hivyo majeshi ya Idi Amin yangepata muda mzuri zaidi wa kujipanga upya kukabiliana na maadui. Lakini Idi Amin hakukubaliana na pendekezo hilo, akitoa hoja kwamba ikiwa watavunja madaraja ili Watanzania wasivuke, hatimaye hata yeye mwenyewe hangeweza kuvuka kuwakimbia majeshi ya Tanzania kutoka kwenye ardhi ya Uganda.
Imani ya Idi Amin ya kuwafukuza majeshi ya Tanzania kutoka Uganda ilikuwa kwa kiongozi wa kijeshi wa Libya, Kanali Muammar Gaddafi. Tangu alipopashwa habari kuwa majeshi ya Tanzania yamevuka mpaka na kuingia Uganda, kila mara alikuwa katika mawasiliano na Gaddafi ambaye aliamini kuwa Uganda ni nchi ya Kiislamu ambayo imevamiwa na jeshi ya nchi ya Kikristo.
Kwa hiyo wakati Amin akikataa wazo la askari wake la kuvunja madaraja nchini kwao—kama walivyovunja lile la Mto Kagera—alikuwa tayari amepata ahadi kutoka kwa Gaddafi kwamba alikuwa anamwandalia askari na silaha ambao wangetumwa Uganda kupambana na Watanzania. Hii ilimpa Amin matumaini mapya. Sasa aliamini kuwa hatimaye ushindi ungekuwa upande wake. Kwa hiyo hakukuwa na sababu yoyote ya kuharibu madaraja mazuri ambayo wangelazimika tena kuyajenga baada ya Tanzania kushindwa vita.
Hadi kufikia wakati huu askari wa Libya walikuwa hawajaonekana vitani Uganda. Walioonekana ni Wapalestina waliokuwa wamevaa skafu za PLO na wengine walibeba vitambulisho. Jumanne ya Machi 13, 1979, kupitia Redio Uganda, Idi Amin alitangaza hadharani kuhusu ushiriki wa PLO kwamba, “majeshi ya Palestina yanapigana bega kwa bega mstari wa mbele.”
Kitendo cha Idi Amin kutangaza hadharani kiliwafanya PLO kushindwa kukanusha. Lakini walijaribu kujinasua. Walisema mamia ya watu wao waliopo Uganda walikuwa huko kwa ajili tu ya mafunzo ya kijeshi na si zaidi ya hapo. Lakini hawakuweza kukanusha kama walikuwa wanapigana bega kwa bega na majeshi ya Amin.
Hata hivyo PLO walifadhaika kiasi kwamba waliamua kutuma ujumbe wao mjini Dar es Salaam kusisitiza uhusiano mzuri na mwema na Tanzania. Jumatano ya Machi 21, 1979 ujumbe huo ukaitisha mkutano na waandishi wa habari na kusema, “Hakuna Mpalestina anayepigana bega kwa bega na majeshi ya Idi Amin.”
Lakini hilo halikuondoa ukweli kwamba ushiriki wa PLO katika jeshi la Amin ulikuwa mkubwa. Pamoja na ukweli huo, Rais Nyerere hakuvunja uhusiano kati ya Tanzania na PLO. Ni wakati gani askari wa Libya walliingia.
Tukutane toleo lijalo.