Kuingia ndani ya Uganda ilikuwa ni awamu ya pili ya Vita vya Kagera. Kabla awamu hiyo haijaanza, kulifanyika mabadiliko ya uongozi kwenye uwanja wa vita. Baada ya kufanya kazi kwa muda wa miezi mitatu akiwapanga wapiganaji wa JWTZ na kuirejesha ardhi ya Tanzania iliyotekwa na Idi Amin, Brigedia Jenerali Tumainieli Kiwelu alirejeshwa Dar es Salaam. Kazi ya kuingia Uganda ikaenda mikononi mwa kamanda mwingine, Meja Jenerali David Msuguri.
Ilipangwa miji ambayo ingeanza kutekwa ambayo ni Masaka na Mbarara. Hii ikabatizwa jina la Mapigano ya Masaka ambayo ilidumu kwa siku mbili tu; Ijumaa na Jumamosi ya Februari 23 na 24, 1979 na ikamalizika.
Lakini kabla Masaka haijafikiwa kulikuwa na miji midogo midogo ya kutekwa. Mmojawapo ni Lukoma ambako kuna uwanja mdogo wa ndege uliojengwa mahsusi kwa shughuli za kivita na ni umbali wa kilomita 20 kutoka mpaka wa Tanzania.
Ndege za kijeshi zilizoishambulia Tanzania zilipaa kutoka katika uwanja huo uliozungukwa na vilima vya Nsambya, Kikandwa na Simba. Vilima vyote hivi askari wa Idi Amin walikuwa wametanda wakiwa na silaha kali za kivita vikiwamo vifaru na mizinga mikubwa.
Brigedi tatu zilizokamilika 201, 207 na 208 zilitumwa kuingia Masaka. Mpango wa awali ulikuwa ni kuzitumia brigedi za 201 na 208 kushambilia vilima vya Simba kutokea Kusini-Magharibi na Brigedi ya 207 ishambulie kutokea Mashariki.
Lakini baadaye taarifa za kiintelijensia zilisema kulikuwa na zaidi ya askari 500 wa Idi Amin wakiwa na vifaru na mizinga mikubwa eneo la Katera kwenye rasi ya Sango Bay, eneo la Kakuuto upande wa pili wa Ziwa Victoria. Kuwaacha hawa ingefanya eneo la upande huo wa Tanzania kuwa hatarini zaidi kushambuliwa.
Kwa hiyo iliamuliwa Brigedi ya 207 ianze kushambulia Katera. Kulikuwa na njia mbili za kufika Katera kutokea Minziro. Njia ya kwanza na rahisi zaidi ilikuwa ni barabara kuu, lakini kwa kutumia njia hiyo jeshi la Tanzania lingekutana na mashambulizi ya uso kwa uso kutoka jeshi la Idi Amin.
Njia ya pili na ngumu zaidi ni kupita kwenye uchochoro wenye mabwawa yaliyojaa maji kutokana na mvua iliyokuwa ikinyesha. Huu ni upande wa pili wa Ziwa Victoria.
Askari wachache waliozaliwa katika vijiji vilivyozunguka ziwa karibu na Bukoba na ambao walijua lugha na tamaduni za eneo hilo walichaguliwa wasonge mbele, wakivalia nguo za kiraia na kubeba matairi ya baiskeli na bidhaa nyingine kama vile wanakwenda sokoni. Askari waliobaki nyuma wakawafuatilia kwa kufuata nyayo zao.
Siku iliyofuata walirudi wakiwa wamechoka kupita kiasi na wengine wakiwa wagonjwa. Waliripoti kuwa mvua kubwa iliyonyesha iliharibu sana barabara kiasi cha kutopitika.
Pamoja na ripoti ya wanajeshi hao, Kamanda wa brigedi hiyo, Brigedia John Butler Walden, aliamua ni lazima wasonge mbele hata kama hali ya hewa ni mbaya kiasi gani. Huyu ni brigedia aliyeitwa ‘Black Mamba’.
Kwa kuwa alijua wanajeshi wake wasingepata moyo wa kusonga mbele bila yeye kwenda nao bega kwa bega, aliamua kutembea nao kwa mwendo wa zaidi ya kilomita nane za kwanza kutoka Minziro hadi kilima cha Bulembe.
Brigedia Walden alidhani mwendo kwa hizo kilomita nane ungewachukua saa chache kupita kwenye msitu mnene, lakini iliwachukua karibu saa 11 wakipambana na matope, madimbwi makubwa ya maji, mbu na mbung’o na maeneo mengine walilazimika kutembea kwenye madimbwi ya maji yaliyowafika mabegani karibu kabisa na kuzama.
Hatimaye walipofika eneo ambalo lilikuwa kavu kwa kiasi fulani, Brigedi ya 207 ilipumzika kidogo kisha ikaanza tena matembezi marefu kuelekea Kaskazini umbali wa kilomita 28 kuingia ndani ya Uganda katika mji wa Katera.
Walipodhani masaibu yamekwisha, ndipo yalipoongezeka. Wadudu kama mbu na mbung’o wakaongezeka. Brigedi ya 207 ikajikuta katika vita ya aina mbili kupambana na jeshi la Idi Amin na wadudu wanaokera katika msitu mnene, huku mvua ikinyesha na barabara yenye madimbwi kujaa maji.
Silaha walizokuwa nazo zikalowa maji. Kutokana na barabara kutopitika kwa gari hata zile gari za jeshi askari wa brigedi hii walilazimika kubeba vichwani mwao silaha zao na zana zingine za kivita.
Hatari kubwa zaidi kuliko mbu na mbung’o ilikuwa ni wanyama kama mamba na viboko waliokuwa maeneo hayo, hususan kuelekea Sango Bay. Kwa hiyo kulikuwa na hofu nyingine ya wanajeshi hao kushambuliwa na hata kuliwa na wanyama hao wakali.
Kwa umbali wa kilomita 28, na kutokana na ubovu mkubwa wa njia waliyopita ikiwa na madimbwi makubwa yaliyojaa maji, ikijumlishwa na mashambulizi ya wadudu, brigedi hiyo ilitumia muda wa saa zaidi ya 50 bila kupumzika wala kula.
Redio za mawasiliano walizokuwa nazo zililowa maji hata zikashindwa kufanya kazi. Kwa hiyo walipoteza mawasiliano kabisa na makao makuu ya kikosi chao.
JWTZ ilianza kuwatafuta wanajeshi hao bila mafanikio. Kukawa na hofu kubwa kuwa Brigedi ya 207 imeshambuliwa na kufyekwa yote. Hakukuwapo na namna yoyote ambayo yeyote katika brigedi hiyo angeweza kufikiwa.
Hatimaye ilipofika saa 11 jioni ya siku ya tatu, brigedi hiyo ikaibuka kutoka kwenye mabwawa ya maji na matope. Angalau sasa redio zikaanza kufanya kazi na wakaweza kuwasiliana na kituo chao cha kazi.
Ingawa hakuna mwanajeshi hata mmoja aliyepoteza maisha, zaidi ya 200 miongoni mwao walikuwa wagonjwa na wachovu mno kiasi kwamba walishindwa kusonga mbele. Wengine walifikia hatua ya kushindwa hata kutembea kiasi kwamba ilitumwa helikopta ya jeshi kuwabeba.
Kwa kuwa wanajeshi wa JWTZ walikuwa wamechoka sana, iliamuliwa kuwa wasubiri hadi kupambazuke ndipo mashambulizi yaanze. 

Majeshi ya Tanzania yashambulia vilima vitatu Uganda


KABLA ya kupambazuka askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) walianza kushambulia vilima vya Kikanda, Nsambya na Simba. Majeshi ya Idi Amin yalijua wanajeshi wa Tanzania wangeingia Uganda kushambulia, lakini hawakujua kwa hakika shambulio hilo lingefanyika lini na wapi na kwamba lingefanyika kutokea upande gani.
Kwa jinsi mashambulizi yalivyokuwa makali na ya kushtukiza, Redio Uganda ilitangaza kuwa Uganda imevamiwa na majeshi ya Tanzania na Cuba. Ingawa Cuba ilikanusha habari hizo, Idi Amin aliendelea kuzisisitiza kiasi kwamba jarida la To the point international liliandika, “Dikteta wa Uganda anapiga kelele”.
Kwa mujibu wa kitabu cha War in Uganda, usiku mmoja kabla ya kushambulia vilima vya Simba, baadhi ya makamanda wa brigedi walikutana kwa mazungumzo na kupata kinywaji. Kwa wakati wote huu, kila upande—Tanzania na Uganda—ulikuwa ukijaribu kunasa mawasiliano ya upande wa pili.
Baada ya kupata kinywaji, makamanda wa brigedi walirejea katika vituo vyao na kuanza kucheza kitimbi. Kwa mujibu wa kitabu hicho, makamanda hao walianza kuwasiliana wenyewe kwa wenyewe kwa kutumia redio za upepo.
Mmoja akauliza, “Wacuba wameshakaa tayari upande wa kulia?” Halafu akajibiwa na askari mwingine: “Tayari afande.” Yule wa kwanza akauliza tena, “Waisraeli wameshajiweka tayari upande wa kushoto?” Halafu akajibiwa, “Wako tayari afande.” Kisha akaendelea, “Na je, Wamarekani nao wameshakaa tayari eneo la kati?” Akajibiwa, “Wako tayari afande.” Kisha akasema, “Haya. Twende kazi.”
Majeshi ya Idi Amin yalikuwa yanafuatilia mawasiliano hayo ya redio. Baada ya kusikia mawasiliano hayo, ndani ya dakika chache majeshi ya Uganda yakaanza kulikimbia eneo hilo mmoja baada ya mwingine.
Katika mawasiliano ambayo JWTZ iliyanasa kutoka Uganda walisikia kamanda wa vikosi vya eneo hilo akiwasiliana na makao makuu mjini Kampala akisema, “I see! Kweli wanakuja sasa.” Kisha sauti kutoka Kampala ikajibu, “Sawa. Wapigeni.” Kamanda aliyekuwa akiongea katika mawasiliano hayo alikuwa eneo la vita akiwasiliana na aliyepo makao makuu mjini Kampala. Alipoambiwa wapigeni, yeye akajibu, “Tubadilishane. Wewe njoo huku (vitani) na mimi nije huko (ofisini).”
Siku iliyofuata Idi Amin, kwa kuyaamini maneno ya makamanda wa brigedi waliotaja Wamarekani, Waisraeli na Wacuba, aliingia kwenye studio za Redio Uganda na kuanza kutangaza kuwa nchi yake imevamiwa na Watanzania, Waisraeli, Wacuba na Wamarekani.
Kusikia taarifa hizo, vyombo vya habari vya dunia vikashangazwa na madai ya Amin. Ingawa ilikuwa ni uongo kuwa kulikuwa na Wacuba, Waisraeli na Wamarekani walioivamia Uganda, ukweli ni kwamba Idi Amin alizipata habari hizo kutoka kwa wanajeshi wake ambao nao waliamini kile kitimbi kilichochezwa na makamanda wa JWTZ.
Ni kweli kwamba makamanda wa JWTZ ndio waliosema hayo, na hayo waliyoyasema yakanaswa na redio za mawasiliano za jeshi la Amin ambalo baada ya kuziamini walizipeleka kwa Amin ambaye naye aliziamini na kuitangazia dunia.
Lakini Meja Jenerali David Msuguri, ambaye kwa sasa ndiye alipokea kijiti kutoka kwa Brigedia Jenerali Tumainieli Kiwelu kushambulia majeshi ya Amin, alikemea kitendo cha makamanda hao. Hata hivyo kitimbi hicho kilifanikiwa sana kwa sababu kiliyatia kiwewe majeshi ya Amin.
Mashambulizi makali yakafanywa na JWTZ katika vilima vya Kikanda, Nsambya na Simba. Majeshi ya Idi Amin yalielemewa katika maeneo hayo. Mizinga mikubwa ya Tanzania ikavunja nguvu ya jeshi la Amin.
Upande wa Kaskazini mwa vilima ambako majeshi ya Amin yangeweza kupata mwanya wa kukimbia ulikuwa umezingirwa na brigedi za 201 na 208. Majeshi ya Amin hayakujua yalivyozingirwa.
Walishtukia tu wanashambuliwa na wakastaajabu zaidi kuwa hata walikokuwa wanakimbilia nako kulikuwa kumezingirwa na wapiganaji wa JWTZ. Katika shambulizi hilo moja la siku hiyo moja peke yake, kiasi cha wanajeshi 250 wa Idi Amin waliuawa.
Walipochunguza maeneo waliyoshambulia, makamanda wa Tanzania walitambua kuwa wenzao wa Uganda hawakujua namna ya kutumia vizuri maeneo yaliyoinuka kukabiliana na adui.
Katika kilima cha Nsambya, JWTZ ilikuta handaki moja na simu moja tu ya mawasiliano. Katika eneo la kilima cha Kikanda Watanzania walistaajabu sana walipogundua mizinga mikubwa ambayo makombora yake ndiyo yaliyokishambulia kikosi cha Luteni Kanali Salim Hassan Boma eneo la Mutukula, ilikuwa nyuma ya mlima badala ya juu ya mwinuko.
Wakati mapambano yakiendelea kwenye vilima hivyo, ndege za kivita za Amin zilijaribu kusaidia wanajeshi wake lakini bila mafanikio. Ndege hizo zilishindwa kuokoa jahazi kwa sababu kufikia wakati huo ndege nyingi za Uganda zilikuwa zimeshatunguliwa na JWTZ.
Tangu wapiganaji wa JWTZ walipovuka mpaka na kuingia ardhi ya Uganda Jumamosi ya Januari 20, 1979 na kuteka vilima vilivyotajwa hapo juu pamoja na kiwanja cha ndege za kijeshi cha Lukoma kilichoangukia mikononi mwa JWTZ Jumanne ya Februari 13, Tanzania ilikuwa imeshaangusha ndege 19 za Jeshi la Uganda.
Kilichoanza kumkatisha tamaa Idi Amin ni ile kasi ya Tanzania kuangusha ndege za jeshi lake. Kilichomtia kiwewe zaidi ni kasi ya kukamata silaha kutoka kwa majeshi yake. Baadhi ya marubani waliosikia ndege zao zilivyokuwa zikitunguliwa na majeshi ya Tanzania waliingiwa na kiwewe na hivyo wengine walitoroka kazini.
Kilichofanya Jeshi la Anga la Uganda lifikie katika hali mbaya kiasi hicho ni upungufu—na pengine ukosefu wa wataalamu, upungufu wa vipuri vya ndege na marubani wa ndege za kijeshi kukimbia.
Kwa hiyo wakati mji wa Masaka ukianguka mikononi mwa JWTZ tayari Jeshi la Anga la Idi Amin lilikaribia kuwa mahututi.
Hata hifadhi yake ya silaha nayo ilianza kuwa na mushkeli. Kwenye kilima cha Simba, JWTZ ilikamata vifaru sita.
Baadaye vifaru hivyo vilianza kutumiwa na jeshi la Tanzania. Silaha mbalimbali kuanzia bunduki za kawaida hadi mizinga mikubwa ilikamatwa eneo hilo.
Baada ya kukamilisha kazi ya kuteka vilima vya Kikanda, Nsambya na Simba sasa njia ikawa imesafishwa tayari kwa kuushambulia mji wa Masaka. Nini kilitokea?