Miezi miwili ya mwanzo wa vita ilikuwa ni ya kuongeza idadi ya wanajeshi jeshini. Katika lile juma la kwanza vikundi vya wanamgambo vilianza kufanya mazoezi baada ya saa za kazi.
Miongoni mwa wanamgambo hawa walikuwamo wakulima wadogo na wale ambao hawakuwa na ajira. Jeshi la Polisi lilichangia askari wake kiasi cha 2,000.
Juma moja baada ya uvamizi wa Uganda wakuu wa mikoa yote 20 ya Tanzania walikutana mjini Dodoma kujadiliana kuhusu uandikishaji wa wapiganaji. Kila mkoa ulipewa idadi ya kikomo cha wapiganaji 2,000 na wakuu hao walipewa maelekezo ya kuwapokea wale tu ambao walikuwa wamehitimu mafunzo ya mgambo.
Pamoja na hayo, mkuu wa Mkoa wa Mara alipotangaza mkoani mwake kuwa yeyote ambaye anataka kujiunga na jeshi ajitokeze, wananchi wengi walimiminika kwenye vituo vya kuandikishwa. Vituo vya kijeshi mkoani Mara vilielemewa na idadi kubwa ya waombaji, mwishowe Rais Nyerere alikwenda mwenyewe mkoani humo kulikabili tatizo hilo.
Hatimaye mkoa huo ulikubaliwa kuandikisha wapiganaji 4,000 badala ya 2,000 wa kikomo waliokubaliwa awali, ilimradi tu hawakuwa na tatizo la akili, wana elimu ya angalau darasa la saba na ni wanachama wa CCM.
Kwa kutumia utaratibu huo wanamgambo 40,000 waliingizwa jeshini na kufanya idadi ya wapiganaji kufikia 75,000—au zaidi. Hatimaye wapiganaji 45,000 wa Tanzania wakaingia Uganda.
Ingawa wanamgambo wanawake nao walipata mafunzo ya kijeshi sawasawa na wale wa wanaume, hakuna mgambo mwanamke aliyeingia jeshini kupigana vita isipokuwa tu wale waliotumika kama wauguzi.
Mara baada ya uvamizi wa Kagera, Tanzania ilianza kuwahamasisha Waganda waliompinga Idi Amin kupigana dhidi ya Idi Amin. Kufikia hatua hii, mkataba wa Mogadishu— ambao ulilitaka jeshi letu kukaa umbali wa kilomita 16 au zaidi kutoka kwenye mpaka wa Uganda—ukawa umekufa rasmi.
Mkataba huo ulioitwa ‘Mazungumzo ya Mogadishu’ uliafikiwa nchini Somalia Alhamisi ya Oktoba 5, 1972. Ulikuwa ni sehemu ya usuluhishi wa mgogoro kati ya Tanzania na Uganda. Somalia iliepusha vita kati ya Tanzania na Uganda kwa miaka sita tangu 1972 hadi ilipokuja kuzuka baadaye mwaka 1978 na sasa, wakati vita inaendelea, ukawa hauna kazi tena.
Walioshiriki katika mazungumzo hayo ni mawaziri wa mambo ya nje ambao ni John Samuel Malecela (Tanzania), Joshua Wanume Kibedi (Uganda) na Umar Arteh Ghalib au Omer Carte Qalib (Somalia). Mwingine aliyeshiriki ni Katibu Mkuu wa OAU, Nzo Ekangaki.
Kufikia hatua hii Rais Nyerere alisema waziwazi kuwa anaunga mkono wanaompinga Idi Amin na kwamba angetoa mafunzo, silaha na fedha kwa Waganda wowote ambao wangekuwa tayari kwenda Uganda kumpiga.
Wito huo uliitikwa na makundi mbalimbali. Wengine walikuwa wanaishi nchini Tanzania, Kenya, Zambia, nchi za Ulaya na Amerika pamoja na Waganda waliokuwa ndani ya Uganda kwenyewe.
Baadhi ya hawa hawakuwa wapiganaji. Wengine walikuwa wafanyabiashara, walimu au waandishi wa habari. Kwa hiyo hawakuwahi kubeba silaha wakati wowote.
Sehemu kubwa ya hawa ilitokea Tanzania, hususan kwenye kambi ya wakimbizi ya Tabora.
Wengi wao walikuwa katika jeshi la Obote, lakini tangu waliposhindwa katika jaribio lao la mwaka 1972 la kumwangusha Idi Amin hawakuendelea tena kupata mafunzo ya kijeshi.
Baadhi ya wengine hawangeweza tena kuingia kwenye mapambano ya kivita kwa sababu ya uzee.
Hata hivyo, siku chache baada ya uvamizi wa Idi Amin, Obote ambaye alikuwa amekwenda Zambia, alirejea Tanzania haraka na kuanza kuwakusanya makomandoo wa kijeshi kutoka Dar es Salaam na kwingineko.
Wanajeshi wote wa zamani wa Uganda walitakiwa kukutana Tabora kwa mkakati maalumu dhidi ya Idi Amin. Ndani ya wiki moja tu ya wito huo wakakutana 800 chini ya Kanali Tito Okello, ambaye ndiye alikuwa kamanda wa lile jaribio la mapinduzi la mwaka 1972.
Kufikia katikati ya Novemba 1978 kiasi cha wapiganaji 300 miongoni mwao wakawa wamepewa sare za kijeshi na kupelekwa Mwanza ambako walikutana na wenzao wengine ili wapelekwe vitani Uganda.
Mwalimu Nyerere alitaka kikosi cha Waganda hao kiende vitani haraka iwezekanavyo, lakini Obote akapinga akidai kikosi chake cha Tabora kimeganyika na kilihitaji muda kuwekwa sawa. Lakini wengine walisema Obote alihisi kikosi hicho kinamtii zaidi Kanali Okello kuliko yeye.
Okello na wapiganaji wengi walikuwa wa kabila la Acholi na ingawa wakati mmoja Obote alidai kuwa watu hao wa Tabora walikuwa watiifu kwake, wakimbizi wengi wa kabila la Acholi waliona kuwa Obote aliwapuuza wakati wa utawala wake kabla ya kupinduliwa na Idi Amin mwaka 1971.
Wengi wao walikuwa wakidai kuwa wakati Obote akiwa madarakani aliwapendelea watu wa kabila lake la Langi kwa kuwapa ajira na fursa nyingine ambazo wao walinyimwa.
Hata hivyo Nyerere alimsikiliza sana Obote na hivyo aliamuru wapiganaji 300 waliokuwa wameshawasili Mwanza warudi Tabora ambako Obote na Okello wangekubaliana kuwa hao wawe kwenye batalioni moja. Kwa mujibu wa kitabu cha War in Uganda, Tanzania iliwapatia silaha na makamanda wa Uganda wakaanza kutoa mafunzo mara moja.
Wakati huohuo, Nyerere alianzisha kambi ya mafunzo ya Uganda huko Tarime karibu na Musoma. Ilikuwa na uwezo wa kutoa mafunzo kwa wapiganaji 1,200. Nyerere aliwataka Waganda wengine, akiwamo Robert Serumaga na Roger Makasa.
Wengine ni Andrew Adimola wa chama cha Ugandan Redemption and Reconciliation Union. Robert Bellarmino Serumaga ambaye alikuwa mwandishi, aliukimbia utawala wa Idi Amin mwaka 1977. Adimola alikuwa waziri kabla hajakimbia. Mwingine ni Aleker Ejalu. Nyerere aliwasihi wote hawa wahamasishe wapiganaji.

Nyerere ahaha kutafuta marafiki na silaha


Hadi ilipofika Krismasi mwaka 1978, zaidi ya wafuasi 50 wa watu hawa wakawa wamewasili. Wiki chache baadaye wakawasili wengine zaidi ya 100 tayari kwa mafunzo.
Januari 1979 Serumaga na Ejalu walimwambia Nyerere kuwa katika miji ya Kampala na Jinja kuna maelfu ya wanajeshi wanaompinga Idi Amin na kwamba wakipata msaada kidogo tu wataasi.
Nyerere alikubaliana nao, akaruhusu Waganda 200 wapelekwe Uganda kwa kazi hiyo, 50 kwa ajili ya Serumaga na Ejalu na 150 kwa ajili ya Tito Okello. Lakini walipokaribia ufukwe wa Ziwa Victoria upande wa Uganda baadhi ya mashua zao zilizama, baadhi walifanikiwa kurejea Mwanza.
Muda mfupi baadaye Ejalu na Serumaga wakatuma mashua za doria ziwani, lakini walipowasili karibu na mji wa Jinja wote walikamatwa na kuuawa. Baada ya matukio haya, kambi ya mafunzo ya Tarime ikafungwa rasmi.
Kwa upande wa uchumi wa nchi, bidhaa zilianza kupaa bei. Hii ilitokana na kuongezeka kwa kodi ili kulipia mahitaji ya vita. Novemba 15, 1978, jarida la Africa Contemporary Record 1978-1979 lilimnukuu Waziri wa Fedha wa Tanzania, Edwin Mtei akitangaza kuwa vita vimeifanya Serikali kuongeza kodi kwa bidhaa za walaji.
Vita ilipoanza kupamba moto, Tanzania ilianza kuwatafuta marafiki na washirika wake, lakini ikaonekana kusingekuwa na msaada mkubwa kutoka kwao. Rafiki wa kwanza ambaye Tanzania ilimwona alikuwa ni Jamhuri ya Watu wa China (RPC).
Kwa mujibu wa kitabu cha Routledge Handbook of Chinese Security kilichohaririwa na Lowell Dittmer na Maochun Yu, mwaka 1963 kiongozi wa China, Mao Zedong alianzisha falsafa mpya ya kimkakati aliyoiita “mapinduzi ya dunia”.
Nadharia yake akaiita “Two Middle Areas” (liangge zhongjian didai) ambayo aliamini kuwa katikati ya mataifa mawili makubwa Marekani na Urusi kulikuwa na maeneo mawili makubwa katikati yake. Eneo la kwanza lilikuwa ni baadhi ya nchi za bara la Asia, Afrika na Amerika ya Kilatini ambazo ama zilikuwa tayari zimejipatia uhuru au zilikuwa katika harakati ya kujipatia uhuru.
Kwa kufuata falsafa hiyo, mwaka 1964 Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Watu wa China, Zhou Enlai aliitembelea Tanzania. China ilitoa misaada na mafunzo ya kijeshi. Hadi mwishoni mwa 1978, wakati Vita vya Kagera ilipoanza na kupamba moto, Tanzania ilikuwa imeshapokea misaada na zana mbalimbali za kivita kutoka China.
Katika ukurasa wa 42 wa kitabu hicho, waandishi Dittmer na Maochun Yu wanaandika kuwa katika bara la Afrika, nchi ambayo Mao aliipa ‘kipaumbele cha juu’ ni Tanzania. Kuanzia mwaka 1964 Tanzania ilipewa msaada wa silaha mbalimbali vikiwamo vifaru, ndege vita na mfumo kamili wa usalama.
Kitabu cha China into Africa: Trade, Aid, and Influence kilichohaririwa na Robert I. Rotberg (chapa ya mwaka 2008) katika ukurasa wake wa 159 kinasema “...Zana za kivita kutoka China kwenda Afrika tangu 1966 hadi 1977 ilikuwa ni pamoja na boti za doria, vifaru na ndege za kivita aina ya MiG-17, MiG-19 na MiG-21 kwa ajili ya Tanzania.
Katika ukurasa wa 110 wa kitabu chake, Arms for Africa: Military Assistance and Foreign Policy in the Developing World, mwandishi Bruce Arlinghaus ameandika “China ilitoa (kwa Tanzania) asilimia 60 ya mahitaji yote ya kijeshi...”
Pamoja na historia yote hiyo ya urafiki kati ya Tanzania na China tangu 1964 hadi 1978, Tanzania ilipoiendea kwa ajili ya msaada wa zana za kivita za kupambana na Idi Amin, Jamhuri ya Watu wa China iliiambia Tanzania kuwa haitajihusisha kwa namna yoyote na mgogoro kati ya Tanzania na Uganda. Zaidi ya hilo, China iliishauri Tanzania ikae mezani na Uganda kumaliza mgogoro huo.
Kilichofanywa na Serikali ya China ni kuwasilisha tu zana za vita zilizokuwa zimenunuliwa kabla vita haijazuka lakini hakuna silaha za ziada ambazo China ilitoa hata vipuri. Jeshi la Wananchi wa Tanzania likaanza kutegemea vipuri kama betri za vifaru kutokana na silaha walizoteka kwa majeshi ya Idi Amin.
Kwa upande wa Uganda, zana za kijeshi ambazo ilikuwa ikizipata kutoka Urusi hazikuendelea tena kutolewa. Kufikia katikati ya mwaka 1978 Serikali ya Idi Amin ilikuwa inazidi kutengwa.
“Kati ya 1975 na 1978 Uganda ilipata zana za kivita kutoka Urusi, Libya, Iraq, Uswisi na Libya,” kinasema kitabu cha Arms and Warfare: Escalation, De- escalation and Negotiation (chapa ya 1994) cha Michael Brzoska na Frederic Pearson.
Jumatatu ya Novemba 10, 1975 Idi Amin alitishia kuvunja uhusiano na Urusi ndani ya saa 48 ikiwa hangepata alichokitaka kutoka kwao. Alitishia pia kuwa angemfukuza nchini mwake balozi wa Urusi, Andrei Zakharov.
Aliilaumu Urusi kwa kuingilia mambo yake ya ndani. Pia aliilaumu kwa kumnyima vipuri kwa ajili ya ndege zake za kijeshi aina ya MiG-17 na MiG-21.
“Novemba 11, 1975 Idi Amin akatangaza kuwa Urusi imlete balozi wake mwingine ambaye ‘hana ubeberu’ kama aliyekuwapo,” kinaandika kitabu cha Who Influenced Whom: Lessons from the Cold War cha Dale Tatum.
Katika matangazo ya Redio Uganda, Idi Amin alisikika akifoka, “Mimi si kibaraka na sishurutishwi na yeyote.”
Mara baada ya hapo, kinaandika kitabu hicho, “Urusi waliamua kuvunja uhusiano na Uganda, lakini cha kushangaza Urusi iliurejesha uhusiano huo siku nne baadaye Novemba 15, 1978.”
Huu ni ule wakati ambao Idi Amin alikuwa mwenyekiti wa Nchi Huru za Afrika (OAU).
Uganda ilipovamiwa na makomandoo wa Israel katika kile killichoitwa ‘Operation Entebbe’ au kama ilivyojulikana kwa wengine, ‘Operation Thunderbolt’, Jumapili ya Julai 4, 1976 na ndege zake za kijeshi kuharibiwa vibaya, Urusi iliahidi kuimarisha kikosi cha anga cha Jeshi la Uganda na kuwapa ndege nyingine za kivita.
Kwa ahadi hiyo uhusiano kati ya Uganda na Urusi ukaanza kuimarika tena. Marubani wa ndege za jeshi za Uganda walipelekwa mafunzoni Urusi.
Itaendelea