By William Shao
Siku mbili baada ya kukutana na makamanda wa Jeshi la Wananchi Novemba mosi, 1978, Mwalimu Nyerere alilitangazia Taifa kuhusu “uvamizi wa Idi Amin na uamuzi wa Tanzania wa kumpiga”. Akizungumza na viongozi wa Mkoa wa Dar es Salaam kwenye ukumbi wa mikutano wa Diamond Jubilee jijini Dar es Salaam, Mwalimu Nyerere alieleza uvamizi huo na jinsi Tanzania ilivyoamua kupambana na majeshi ya Idd Amin.
“Nimewaombeni mkusanyike tena hapa niwaelezeni jambo ambalo kwa sasa wote mnalijua. Lakini naona si vibaya nikieleza. Nitajaribu kueleza kwa ufupi.
“Wakati nilipokuwa ziarani Songea kuanzia juma la pili la mwezi uliopita (Oktoba), zilitangazwa habari kutoka Uganda kwamba jeshi la Tanzania limeingia Uganda na limechukua sehemu kubwa na kuua watu ovyo.
“Siku zilipotangazwa habari hizo nilikuwa nimekaribishwa chakula cha jioni na vijana wetu wa jeshi pale Songea, na nikakanusha. Na kwa kweli nikachukua nafasi hiyo kuvishutumu vyombo vya habari vya nje ambavyo vinapenda kutangazatangaza uongo wa Amin,” alisema Nyerere.
“Kila anapotangaza uongo, wao huurukia na kutangaza kama kwamba ni kweli. Huo ndio uliokuwa uongo wake wa kwanza, na aliendelea endelea.
“Baadaye akabadili sura, akaongeza uongo wa pili katika shabaha hiyohiyo kuwa Watanzania wanaua watu ovyo na kwamba wanasaidiwa na majeshi kutoka Cuba. Uongo huo nao tukaukanusha.
ADVERTISEMENT
“Kwa hivyo, alivyozidi kusema habari hizo za uongo tuliendelea kuzikanusha na kuzipuuza. Lakini Alhamisi akatuma ndege za kivita Bukoba. Vijana wetu walizitupia risasi zikakimbia. Siku hiyohiyo ikarudi tena moja, ikaangushwa.
“Ijumaa zikaja ndege eneo la Kyaka. Zikatupa mabomu. Vijana wetu walizitupia risasi, na mbili zikaangushwa.”
Nyerere pia alizungumzia ndege za Tanzania zilizopotea uwanjani wakati zikitoka Dar es Salaam kwenda Mwanza ambazo kutokana na kasi yake zilihisiwa kuwa ni za adui na kutunguliwa. Nyerere alisema Tanzania imechoshwa na uongo huo wa Idi Amin na hivyo wameamua zikionekana ndege za kivita, zitunguliwe.
“Kwa hiyo vijana wetu wamekwishaambiwa kuwa ndege za kivita zikionekana, zipigwe. Kama vile zile za Bukoba na Kyaka zilipigwa, basi na hizi zikapigwa zilipofika Musoma. Walidhani ni za adui. Tukapoteza ndege tatu,” alisema Nyerere.
“Lakini katika mambo ya vita ajali hutokea. Na vijana hawa walishaambiwa ndege zikionekana zipigwe. Wangeziacha? Wanajuaje ni za adui? Kwa hiyo ikatokea bahati hiyo mbaya.
“Matukio haya hatukuyatangaza. Hata kule kupigwa kwa ndege za Amin hatukutangaza. Hatukutangaza kwa sababu hatukutaka jambo lenyewe kulipa uzito mno. Tulisema akiendeleaendelea kuleta ndege zake, tutaendelea kuziangusha kila zinapokuja.
“Uwezo wa kuziangusha upo, na mwenyewe alijua uwezo upo. Ni vizuri akijua yeye. Tulijaribu. Tulikuwa tunaepuka kulipa uzito jambo lenyewe ambalo mwanzo wake ni uongo kabisa wa kuzua.”
Nyerere alisema jinsi Idd Amin alivyoendelea kuidanganya dunia na jinsi Tanzania ilivyomjibu hadi alipoamua kuvamia.
“Sasa Jumatatu ndiyo akaivamia nchi yetu. Akaingiza majeshi yake kwa nguvu, nguvu kubwa. Yakachukua sehemu kubwa. Yakaingia ndani mpaka Kyaka. Hii tukatangaza kwa sababu lilikuwa ni jambo la kweli na yeye kama kawaida yake akakana akasema haikutokea hivyo,” alisema Nyerere.
“Akaendelea kusema kwamba Watanzania ndio wako Uganda, ndio wamechukua sehemu ya Uganda. Akakana ukweli huo. Lakini tukawaeleza jamaa na mabalozi walioko Dar es Salaam kuwa huo ndio ukweli.
“Huyu mtu ameivamia nchi yetu. Sasa jana ametangaza mwenyewe kwamba ni kweli majeshi yake yameivamia nchi yetu na yamechukua sehemu hiyo ya Tanzania iliyoko kaskazini mwa Mto Kagera na kwamba tangu sasa, eti sehemu hiyo ni ya Uganda na itatawaliwa kijeshi kama Uganda inavyotawaliwa.”
Alisema kauli hiyo ya Idi Amin iliisaidia Tanzania kutangaza kutokea kwa uvamizi huo.
“Sasa hiyo ndiyo hali. Tufanye nini! Tunayo kazi moja tu. Watanzania sasa tunayo kazi moja tu—ni kumpiga,” alisema Mwalimu Nyerere.
“Uwezo wa kumpiga tunao. Sababu ya kumpiga tunayo, na nia ya kumpiga tunayo. Tunataka dunia ituelewe hivyo. Kwamba hatuna kazi nyingine.
“Na tunaomba marafiki zetu wanaotuomba maneno ya suluhu, waache maneno hayo. Kuchukua nchi ya watu wengine siyo kwamba majeshi yamekosea njia na kusema kuwa sasa sehemu hiyo umeichukua na kutangaza vita kwa nchi ile nyingine. Si sisi tuliofanya hivyo. Amefanya hivyo mwendawazimu.
“Na amefanya hivyo kwa jambo ambalo aliwahi kutangaza zamani. Aliwahi kusema zamani kidogo kuwa mpaka wa haki wa Uganda na Tanzania ni Mto Kagera, na kuwa siku moja atachukua sehemu hiyo. Ametimiza hivyo.”
Nyerere aliwaomba marafiki wa Tanzania kuielewa hali hiyo na kuisaidia katika kuyaondoa majeshi ya Uganda na kwamba wale waliokuwa wakitaka suluhu haitawezekana.
“Hatukupenda kufanya hivyo. Maadui zetu ni mabeberu, na kwa hivi sasa wako Kusini. Serikali ya Afrika, hata kama hatupendi matendo ya viongozi wao, hatuwahesabu kama adui wetu,” alisema Nyerere.
“Na kama Amin angekuwa amesema tu kwamba Tanzania ni adui wetu, sisi tungeendelea kumpuuza kama ni maneno hayo. Lakini kafanya kitendo cha uadui, hatuwezi.
“Ameingia Tanzania mwenyewe. Na mtu huyu ni mshenzi. Ameua watu wengi sana. Kwa hiyo nasema tuna kazi moja tu. Tutampiga. Vijana wetu wako mpakani sasa hivi. Wako kule. Wako kule na mapambano yanaendelea.
“Sasa hayo si mapambano ya TPDF peke yake, ni yetu wote. Kwa hiyo ninachowaombeni wananchi, hiyo kazi iliyoko mbele yetu muielewe.
“Pili, tuwasaidie vijana wetu. Kila mtu kwa mahali alipo. Tutaendelea na kila mapambano yanavyoendelea kueleza nini la kufanya na nani afanye nini.
“Tutaelezana wakati wote huo mpaka tumemuondoa huyu nyoka katika nyumba yetu. Na tunawaomba mtulie. Katika mambo haya ya vita, na hasa kama watu mlikuwa mmezoea amani mnaweza kubabaika sana.
“Msibabaike, tulieni. Fanyeni kazi kama kawaida. Lakini mjue vitendo hivyo kazi yake ni hiyo moja; kumpiga mshenzi huyu aliyekuja katika nchi yetu.”

Idi Amin avunja daraja la Mto Kagera



Baada ya amri ya Rais Julius Nyerere aliyoitoa Jumatatu ya Oktoba 30, 1978 ya kutaka Jeshi la Wananchi (JWTZ) kuingia vitani, Brigedi ya Kusini ilipewa jukumu la kuanza kujibu mashambulizi.
Brigedi ya Kanda ya Kusini iliyokuwa na makao yake huko Songea, chini ya Brigedia James Luhanga, ilikuwa na wapiganaji kati ya 4,000 na 5,000. Kwa mujibu wa gazeti The Citizen la Oktoba 14, 2014, halikuwa jambo la bahati mbaya kwamba brigedi hiyo kuwa tayari kwa vita.
“Brigade hii ilikuwa imeandaliwa ili baadaye iweze kutumwa nchini Namibia kujiunga na askari wa msituni wa Swapo,” linaandika gazeti hilo.
Brigedi hiyo ilianza safari Alhamisi ya Novemba 2, 1978, siku ambayo Mwalimu Nyerere alikuwa akilitangazia taifa kuhusu “uvamizi wa Idi Amin na uamuzi wa Tanzania kumpiga”.
Askari wa brigedi hiyo walilazimika kusafiri na zana zao za kivita kwa umbali wa kilometa 1,600 kutoka Songea hadi uwanja wa vita.
Baada ya safari hiyo ya tabu kubwa kutokana na mvua iliyokuwa inanyesha na barabara kuharibika vibaya, wanajeshi waliwasili na mara moja kuanza kuchimba mahandaki kwa ajili ya kujihifadhi kwa shambulizi lolote la anga ambao halikutarajiwa.
Mjini Dar es Salaam, Waziri Mkuu Edward Moringe Sokoine alitoa maelekezo kwa wakuu wote wa mikoa 20 ya Tanzania kuhamasisha matumizi ya mali za serikali na za watu binafsi kutumika katika vita.
Mabasi na malori kutoka serikalini na kwa kampuni binafsi yalitumika kupeleka wapiganaji na vifaa kwenye viwanja vya vita. Kwa watu waliokuwa na magari mabovu waliiona fursa hiyo kwa sababu magari yao yalifanyiwa matengenezo.
Ingawa yaliteka eneo la Kagera kwa urahisi, majeshi ya Idi Amin yalihofia sana Jeshi la Tanzania kujibu mapigo. Waandishi wa kitabu cha Deadly Developments, Stephen na Downs Reyna wameandika katika ukurasa wa 117 kuwa kwa kuhofia hilo, wanajeshi wa Uganda waliamua kulipua daraja la Mto Kagera eneo la Kyaka.
Toleo la 348 la jarida New African liliandika kuwa “huu ulikuwa mwanzo wa mwisho wa utawala wake (Idi Amin)” nchini Uganda.
Luteni Kanali Marajani wa Uganda alitumia ndege za MiG kulipua daraja hilo. Kazi hiyo ilifanyika Novemba 1 na 2, lakini walishindwa kuliharibu daraja hilo la Kagera. Wanajeshi wa Tanzania walizirushia makombora na baadhi ya ndege hizo zilitunguliwa. Marubani waliobakia wakavunjika moyo wa kuendelea na kazi hiyo.
Baadaye Marajani akapata wazo la kutumia bomu la kutegwa. Akaenda machimbo ya shaba ya Kilembe, kiasi cha kilometa 225 kwenye milima ya Ruwenzori. Meneja wa machimbo hayo, ambaye alikuwa Mwingereza, alikubali na akatuma timu yake ya wataalamu kwenda kutega mabomu daraja la Mto Kagera.
Usiku wa Ijumaa ya Novemba 3, 1978, wategaji wa mabomu hayo walifika darajani na kufanya kazi hiyo bila kuonekana. Kabla ya kupambazuka daraja likawa limelipuliwa. Mmoja wa wanajeshi wa Uganda aliyekuwa na watega mabomu hayo ni Sajini Kifulugunyu.
Kifulugunyu aliliambia gazeti Daily Monitor la Uganda (Aprili 23, 2016) kwamba wataalamu hao wa mabomu walikuwa watatu, lakini utafiti wa gazeti hilo uligundua kuwa walikuwa wanne—Muitaliano mmoja na Waganda wanne.
Baada ya hapo, ilikuwa ni furaha tele.
“Tulifanya sherehe hapa hadi Kampala. Tuliridhika kuwa Jeshi la Tanzania halingeweza kutushambulia tena baada ya kuharibu daraja ambalo wangetumia kuvuka na kuingia Uganda,” Kifulugunyu aliliambia gazeti hilo.
Mmoja wa marubani waliotumika kujaribu kulilipua daraja hilo ni Meja John Amunga (maarufu kwa jina la Kassim Semugabi). Alikuwa mmoja wa marubani bora zaidi wa kijeshi wa Jeshi la Uganda, akiendesha ndege aina ya MiG-21. Wanajeshi wenzake walimbatiza jina la “Mharibifu wa Tanzania”.
Mwingine alikuwa ni John Carse kutoka Seychelles na ambaye alikuwa ni mtaalamu wa ubomoaji. Ndiye anayedaiwa kuwa alilipua daraja hilo.
Lakini, katika ukurasa wa 149-150 wa kitabu cha Guardian Angel: The Moshi Conspiracy kilichoandikwa na Arnold Spero Bisase, kuna maelezo tofauti.
Aliyekuwa mfungwa wa Tanzania ambaye hakutaka jina lake litajwe, na ambaye wakati kitabu hicho kinaandikwa mwaka 2012 alikuwa anaishi nchi za Scandinavia, alimwambia mwandishi wa kitabu hicho kuwa aliwahi kuwa katika gereza moja na John Carse mkoani Dodoma ambako aligundua kuwa raia huyo wa Seychelles hakuhusika kulipua daraja hilo.
Siku daraja hilo lilipolipuliwa, JWTZ ilikumbana na kikwazo kingine. Ndege zake tatu zilikuwa zikitoka uwanja wa ndege wa Ngerengere mkoani Morogoro kuelekea Mwanza, zikapita juu ya Ziwa Victoria ambako askari wa JWTZ walishaambiwa wakae chonjo.
Kitengo cha Musoma hakikuwa na taarifa ya kuwasili kwa ndege hizo. Ndege zote tatu zililipuliwa kwa makombora na kuua marubani wake.
Akilitangazia Taifa tukio hilo, kwa masikitiko Mwalimu Julius Nyerere alisema: “Katika mambo ya vita ajali hutokea, na vijana hawa walikwishaambiwa ndege zikionekana zipigwe. Wangeziacha? Wanajuaje ni za adui? Kwa hiyo ikatokea bahati mbaya hiyo.
“Matukio haya hatukuyatangaza. Hata kule kupigwa kwa ndege za Amin hatukutangaza. Hatukutangaza kwa sababu hatukutaka jambo lenyewe kulipa uzito mno. Tulisema akiendeleaendelea kuleta ndege zake, tutaendelea kuziangusha kila zinapokuja.”
Mara baada ya maneno hayo, alipanda ndege kwenda Beira, Msumbiji kukutana na Rais Samora Machel na kushauriana juu ya uvamizi wa Idi Amin. Nyerere alimwambia Machel kuwa kikosi cha Jeshi la Tanzania kilichokuwa kwenye mpaka wa Msumbiji na Rhodesia (Zimbabwe) kilirudi Tanzania kwa ajili ya Vita ya Kagera.
Itaendelea kesho