Kwa kuwa kila chenye mwanzo hakikosi kuwa na mwisho, Vita ya Kagera nayo ilikuwa na mwisho wake. Ilimalizika hatimaye. Lakini haikumalizika Aprili 11, 1979 baada ya kukombolewa kwa jiji la Kampala, bali ilimalizika Juni 3, 1979 kwa kukombolewa kwa mji wa Arua, ambao ni nyumbani kwa Iddi Amin.
“Juni 3, (1979) majeshi ya Tanzania yalifika kwenye mpaka wa Uganda na Sudani, na vita ikaonekana imemalizika,” kinasema kitabu ‘Arms and Warfare: Escalation, De-escalation, and Negotiation’ cha Michael Brzoska na Frederic Pearson.
“Utawala wa kifashisti wa Iddi Amin ulikoma Aprili 11, (1979) baada ya Jiji la Kampala kuanguka (lakini vita haikumalizika baada ya kutekwa kwa kampala.) Baada ya kukamatwa kwa mji wa Arua, kijiji cha nyumbani kwa Amin Juni 3, vita iliyodumu kwa miezi tisa ikamalizika,” kinaandika kitabu ‘From Jerusalem to the Lion of Judah and Beyond: Israel’s Foreign Policy in East Africa’ cha Steven Carol.
Jarida ‘America and the World 1979’ likaandika baada ya mji wa Arua kunyakuliwa “vita ikatangazwa kumalizika rasmi.”
Hadi kufikia Jumapili ya Juni 3, 1979, wanajeshi wa Tanzania walikuwa wameshatembea kilomita 12,000 kwenye uwanja wa vita tangu ilipoanza Oktoba, 1978. Tanzania ilishinda vita hiyo na kumwondoa Amin madarakani, lakini ikabakiwa na gharama kubwa za kulipa.
Gharama ambayo Tanzania ilitumia katika vita hiyo ni dola milioni 500 za Marekani. Waandishi wa kitabu ‘Development Centre Studies: Conflict and Growth in Africa Kenya (Volume 2)’, Klugman Jeni, Neyapti Bilin na Stewart Frances katika ukurasa wa 72 wameandika:
“Vita dhidi ya Uganda iliongeza matumizi kwenye usafiri na ulinzi kutoka asilimia 12.3 (za pato la ndani) za mwaka 1976/77 hadi asilimia 24.4 katika mwaka wa fedha wa 1977/78... Vita ya Uganda iliigharimu Tanzania kiasi cha dola za Marekani milioni 500 (kiasi cha asilimia 15 ya Pato la Taifa la mwaka 1978).”
Kitabu ‘Agriculture in Tanzania Since 1986: Follower or Leader of Growth?’ kinasema ingawa uchumi wa Tanzania uliimarika sana mwaka 1976, kuimarika huko kulikuwa kwa muda mfupi tu. Kuvunjika kwa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) mwaka 1977 kulisababisha biashara kudorora, lakini kilichofanya hali kuwa mbaya zaidi ni hii Vita ya Kagera.
Kuanzia hapo, hali nzuri ya uchumi wa Tanzania haikutulia tena. Tanzania “ilizidi kutumbukia kwenye madeni,” kinasema kitabu ‘The Rough Guide to Tanzania’ cha Jens Finke (uk. 719).
“Nyerere alijikuta katika hali ngumu na mawazo yake ya kijamaa. Mbali na siasa ya ujamaa na kujitegemea, Tanzania ikaanza kuwa tegemezi kuliko ilivyokuwa awali. Uchumi ulikuwa umeanguka. Mazao ya kilimo hayakutosheleza mahitaji ya chakula na uchumi ukaelemewa na madeni … theluthi moja ya bajeti yote ya Tanzania ikategemea mikopo kutoka kwa nchi wafadhili na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF),” anaandika Jens Finke katika kitabu chake, ‘The Rough Guide to Tanzania’.
Kitabu ‘War in Uganda: The Legacy of Idi Amin’ kinasema askari wa Tanzania waliouawa katika mapigano kwenye vita hiyo ni 373. Kwa mujibu wa gazeti ‘Daily Monitor’ la Uganda la Jumapili ya Aprili 27, 2014, askari 93 miongoni mwa hao 373 waliuawa na jeshi la adui lakini wengine walifariki dunia kutokana na ajali na majanga ya asili. Jeshi la Umoja wa Kuikomboa Uganda (UNLA) lilipoteza askari wake 150.
Kwa mujibu wa ‘Daily Monitor’, askari wa Libya nao waliokufa kwa wingi katika Vita ya Kagera. Kiasi cha askari 600 miongoni mwa 3,000 waliotumwa kwenda Uganda kumsaidia Amin waliuawa. Lakini waliokufa kwa wingi kuliko askari wa upande wowote ni wale wa Uganda.
Amin alipoteza zaidi ya askari 1,000. Katika ukurasa wa 567, kitabu ‘Warfare and Armed Conflicts: A Statistical Encyclopedia of Casualty and Other Figures, 1492—2015’ cha Micheal Clodfelter kimeandika kuwa “takribani raia 1,500 wa Tanzania na 500 wa Uganda waliuawa” katika vita hiyo.
Raia hao wa Tanzania waliuawa wakati majeshi ya Amin yalipovamia Kagera, lakini raia wa Uganda waliouawa ilikuwa ni wakati vita ikiendelea na waliuawa ama kwa bahati mbaya au kwa makusudi wakati wa mapambano.
Kutokana na ushindi wa Tanzania dhidi ya Amin, Rais wa Tanzania alisema amejifunza mengi sana kuhusu vita kuliko wakati mwingine wowote katika maisha yake. “Nachukia vita sasa kuliko nilivyoichukia siku zote kwa sababu sasa naijua zaidi kuliko nilivyoijua mwanzo,” alisema Nyerere.
Alipoulizwa kuhusu Serikali ya Uganda, Nyerere alisema “Hatupendi kujihusisha sana na mambo ya ndani ya Uganda.” Lakini ukweli ni kwamba alishindwa kuacha kujihusisha kwa sababu bado Serikali ya Uganda haingeweza kufanya chochote bila kumshirikisha.
Kitabu ‘Uganda Since the Seventies’ cha Godfrey Mwakikagile kinamkariri aliyepata kuwa Rais wa Uganda, Godfrey Binaisa akisema: “Kati ya mwaka 1979 na 1980 Nyerere alikuwa (kama) Rais wa Uganda... Hata kama unataka kupiga chafya au kusogeza mguu wako lazima umjulishe Nyerere...”
Lakini pamoja na yote hayo, Watanzania na Serikali yao ndio waliolipa gharama kubwa ya vita hiyo. Ingawa hivyo, Meja Jenerali Benjamin Msuya, ofisa mwandamizi wa JWTZ aliyeiteka Kampala, alisema pamoja na gharama zote hizo vita hiyo ilikuwa ya lazima kupigana.
Alhamisi ya Aprili 12, 2007 gazeti LA ‘Daily Nation’ la Kenya likaripoti kuwa Uganda imeilipa Tanzania dola za Marekani milioni 67 kama fidia ya hasara ambayo iliipata kutokana na vita hiyo.
Gazeti hilo, likimkariri mkurugenzi wa mawasiliano wa Benki Kuu ya Uganda, Juma Walusimbi, akithibitisha kumaliza kuilipa Tanzania deni lake.
Je, Serikali mpya ya Uganda iliweza kuendelea bila kuhitaji msaada wa Tanzania?

VITA YA KAGERA: Yusufu Lule aondolewa madarakani






HAKUNA vita visivyokuwa na gharama. Katika toleo lililopita tuliona gharama ambazo Tanzania na Uganda ziliingia kutokana na vita hiyo. Gharama ambazo Tanzania ilitumia ni Dola 500 milioni za Marekani. Askari wa Tanzania waliouawa katika mapigano kwenye vita hiyo ni 373 na takribani raia 1,500. Askari 600 miongoni mwa 3,000 wa Libya nao waliuawa.
Ingawa vita vilimalizika hatimaye, hali ya kisiasa nchini Uganda haikutulia. Ndani ya siku 68 tu Profesa Yusuf Lule aliondolewa madarakani na Baraza la Ushauri la Taifa (NCC). Sasa endelea...
Wakati vita dhidi ya Iddi Amin ikimalizika, tayari Uganda ilikuwa kwenye mgogoro wa kisiasa. Kumwondoa Amin madarakani lilikuwa jambo moja, lakini kuleta utulivu wa kitaifa lilikuwa jambo jingine.
Profesa Yusuf Lule aliapishwa Ijumaa ya Aprili 13, 1979. Siku chache baada ya kuapishwa alianza kupuuza maazimio yaliyofikiwa kwenye mkutano wao wa Moshi ambayo yaliwekwa kwenye katiba ya Umoja wa Kitaifa wa Kuikomboa Uganda (UNLF).
Katiba ya UNLF haikumpa Rais madaraka makubwa yakiwamo yale ya kuwateua mawaziri wake. Mamlaka makubwa yaliwekwa mikononi mwa Baraza la Ushauri la Taifa (NCC), lakini Lule alitaka mamlaka makubwa awe nayo Rais. Mgogoro ulianzia hapo.
Profesa Lule na washauri wake akiwamo Dk Andrew Lutaakome Kayiira, walianza kufanya uamuzi mkubwa na uteuzi mkubwa bila kuishirikisha NCC wala kupata ridhaa yake.
Matendo hayo yaliwakasirisha sana maofisa wa UNLF na wajumbe wa NCC. Lule aliwajibu kwa kuwaambia kuwa maazimio yaliyopitishwa kwenye mkutano wa Moshi hayakuwa na nguvu ya kisheria na kwamba yeye ataendelea kutekeleza majukumu yake kwa kutumia katiba iliyokuwapo kabla Amin hajatwaa madaraka—katiba iliyotengenezwa na Dk Milton Obote ambayo ilimpa Rais madaraka makubwa.
Lule kupuuza Azimio la Moshi kulianza kuonekana pale aliposhindwa kuhudhuria hafla ya kuapishwa kwa wajumbe wa NCC. Hafla hiyo ilipopangwa kufanyika upya, Lule alihudhuria, lakini baada ya kutoa hotuba fupi aliondoka kabla ya wajumbe kuapishwa, jambo lililowakasirisha zaidi.
Bila kuishirikisha NCC, Lule aliendelea kuwateua mawaziri na manaibu waziri aliowataka yeye. Aliwateua mawaziri 24 na manaibu wake 20 na hao moja kwa moja wakawa wajumbe wa NCC, wakiwazidi kwa idadi wajumbe waliochaguliwa katika mkutano wa Moshi.
Wajumbe wa NCC walikerwa zaidi pale Lule alipowapatia kila waziri wake Dola 5,000 za Marekani kama posho ya ukarabati wa nyumba zao. Walipomuuliza kulikoni akaamua kumpa kila mjumbe kiasi hicho cha fedha kutoka kwenye mfuko wa Serikali iliyofilisika—lakini wajumbe wa NCC waligoma, hakuwa na jibu.
Yote haya yalikuwa yakifanyika wakati Kampala ikiwa katika hali ya hatari. Milio ya risasi ilikuwa ikisikika kila siku hasa usiku na miili ya watu ikiwa inaokotwa kila asubuhi.
Wakati mgogoro kati ya Profesa Lule na NCC ukifikia hatua mbaya, Rais wa Tanzania, Mwalimu Nyerere aliwaita viongozi wa Serikali ya Uganda na kukutana nao Mwanza. Lule naye alifika Mwanza kukutana na Nyerere. Alifuatana na Paulo Muwanga na watu wengine. Walipata chakula cha mchana kilichoandaliwa na Nyerere katika Hoteli ya Mwanza.
Kitabu cha New African Yearbook 1991/92 kinasema katika mabadiliko ya baraza la mawaziri la Lule, kumi kati ya 19 walikuwa ni Wabaganda. Na baada ya kukutana na Nyerere mjini Mwanza alifanya mabadiliko mengine na kuongeza mawaziri sita wengine.
Mara baada ya kupata chakula, Muwanga akapokea taarifa kutoka Kampala kwamba Redio Uganda imetangaza mabadiliko ya baraza la mawaziri na kwamba hata yeye mwenyewe ameguswa. Aliondolewa Wizara ya Mambo ya Ndani akapelekwa Wizara ya Kazi. Hatua hii ilimkasirisha sana Muwanga, kwa mujibu wa kitabu cha UPC and National-Democratic Liberation in Uganda cha Yoga Adhola.
Mwandishi wa kitabu cha Guardian Angel: Volume Two: The Moshi Conspiracy, Dk Arnold Spero Bisase anasema Muwanga aliapa lazima amshughulikie Profesa Lule.
Mabadiliko ya baraza la mawaziri bila NCC kushirikishwa sasa ikaonekana kuwa Lule amekuwa sugu—haambiliki. Waliona kuwa amekuwa na kiburi sana hata akafanya mabadiliko ya baraza la mawaziri wakati ameonywa na Nyerere kwamba akiendelea na tabia hiyo basi yeye (Nyerere) hataweza kumuokoa.
Nyerere alimwambia Lule afuate Azimio la Moshi linalotaka mamlaka makubwa yawe ni ya NCC na si ya Rais. Lule alimsikiliza Nyerere, lakini ni kama hakumsikia.
Ijumaa ya Juni 8, 1979 wajumbe wa NCC waliokuwa na hasira walikutana mjini Kampala na kupitisha azimio la kumtaka Lule akabidhi teuzi zote “haraka sana” kwa NCC ili zijadiliwe na kuidhinishwa.
Siku nne zilipita bila NCC kupata jibu. Wajumbe wakakutana tena na kupitisha azimio jingine lililomtaka Lule atekeleze matakwa yao “mara moja”. Hata hivyo hawakupata jibu.
Jumanne ya Juni 19, 1979 NCC wakakutana tena. Wakati huu hawakukutana Kampala, bali ni kwenye Ikulu ya Entebbe. Walianza mkutano wao saa 9:22 alasiri chini ya mwenyekiti wao, Edward Bitanywaine Rugumayo.
Lule naye alihudhuria mkutano huo. Alipotakiwa kujibu kwa nini alipuuza maazimio ya NCC, alijibu hakufanya hivyo kwa sababu huko kungemaanisha “kuhusisha masuala muhimu ya kikatiba”.
Mjadala mkubwa uliendelea, kwa mujibu wa kitabu cha Upc and National-Democratic Liberation in Uganda. Mazungumzo ya wajumbe wengi ni Azimio la Moshi. Ingawa Lule alijitetea sana, alibanwa.
Alisema hakuwahi kupata mawasiliano yaliyotumwa kwake na NCC, lakini barua ya NCC aliipeleka Rugumayo mwenyewe ofisini kwa Lule.
Muda mfupi baadaye Profesa Paulo Wangoola akasimama. Akatoa hotuba ndefu. Akasema, “demokrasia imewekwa majaribuni ... Uamuzi unafanywa nje ya NCC ... Lule ameibaka UNLF ... Tumefikia mahali pagumu sana. Kuna ombwe la kisiasa. Rais (Lule) haikubali UNLF na hatuwezi kuwa na Rais asiyeikubali UNLF. Ingawa Lule alifanya kazi muhimu kutuleta Kampala, sasa anatukwamisha.”
Wangoola akahitimisha kwa kuleta hoja ya kutokuwa na imani na Profesa Lule. Mjadala mrefu ukaanza na kuendelea hadi usiku wa manane.
Hatimaye ilipohitimu saa saba kamili usiku, kura za siri zikapigwa. Dakika 35 baadaye matokeo yakatangazwa. Wajumbe 18 waliunga mkono hoja, 14 walipinga. Rugumayo akamgeukia Lule na kumwambia kuwa yeye si Rais wa Uganda tena. Baada ya kumwambia hivyo Lule, aliwageukia wajumbe na kusema, “Waliomwodoa Lule (yeye) kwenye kiti chake pia wamewaondoa na mawaziri wake”.
Lule, pamoja na wajumbe wengine tisa wa NCC wakasusa na kuondoka kikaoni. Lule akakoma kuwa Rais wa Uganda cheo alichokitumikia kwa siku 68 tu.