MIAKA 20 BILA NYERERE: Nyerere ashtakiwa kwa kosa la uchochezi-2






Mwaka 1958 Mwalimu Nyerere alishtakiwa kwa kosa la uchochezi kutokana na makala aliyoandika kwenye gazeti la chama cha Tanu lililoitwa ‘Sauti ya Tanu’. Alipatikana na hatia na kuhukumiwa kwenda jela miezi sita au kulipa faini ya Pauni 150 za Uingereza (shilingi 3,000 za Tanzania wakati huo).
Tangu kilipoanzishwa Jumapili ya Julai 7, 1954, chama cha Tanu na rais wake Julius Nyerere, kilianza kuonekana kuwa mwiba mchungu kwa Serikali ya kikoloni. Kama ilivyo kwa harakati zote za kisiasa, Nyerere na Tanu walikabiliana na serikali ya kikoloni chini ya Gavana Edward Francis Twining.
Tanu walikuwa makini kuonyesha makosa yaliyokuwa yakitendwa na Serikali ya kikoloni, jambo lililowakera sana watawala wa kikoloni.
Kwa mujibu wa kitabu ‘A Gust of Plumes: A Biography of Lord Twining of Godalming and Tanganyika’ © 1972, mwaka 1957 Serikali ilipiga marufuku mikutano ya hadhara iliyoendeshwa na Tanu kwa sababu matamshi yake yalichukuliwa kuwa ya chuki kwa serikali.
Lakini kwa kuhofia Umoja wa Mataifa, marufuku hiyo iliondolewa baadaye mwaka huo ingawa Serikali hiyo iliendelea kuwawekea Tanu vikwazo vya kisiasa.
Baada ya Nyerere kukerwa na unyanyasaji wa kisiasa wa Serikali ya wakoloni, Jumanne ya Mei 27, 1958 aliamua kuandika makala katika gazeti la ‘Sauti ya Tanu’ akiwashutumu wakuu wa wilaya wawili kwa kuwaita ni “washenzi na maharamia.”
Ingawa kuna marejeo fulani yanadai kuwa makala hiyo alichapisha Mei 7, 1958, ambayo ilikuwa Jumatano, marejeo mengi yanakubaliana ilikuwa Mei 27 na toleo la gazeti lilikuwa ni namba 29.
Katika makala hayo, kinasema kitabu ‘The Making of Tanganyika’ Judith Listowel © 1965, Nyerere alidai kuwa wakuu hao wa wilaya walikuwa wakifunga matawi ya Tanu Geita na Mahenge na kula njama za kuwaadhibu machifu walioiunga mkono Tanu. Sehemu ya makala hayo inasema: “Jamaa hawa wanawaghilibu watu waape uwongo kortini ili kuisingizia Tanu. Hawa hawa wanawapotosha watu na kuwaadhibu wasiokuwa na hatia. Jamaa hawa wanajidai kuhifadhi sheria na utangamano...
“Hatuiogopi sheria, ikiwa polisi hawajiingizi katika mambo ya siasa na kuamuru kati ya watiifu na wengine pamoja na magavana wa msituni, wanaojidai sheria haiwahusu, hapo basi, sheria inatufaa sana. Sababu za hawa wendawazimu kuwachokoza watu wafanye matata ni kuwa hatushindwi tukiwa watii wa sheria. Njama zao zimewatatanisha wenyewe walipofunga ofisi ya Tanu.
“Ikiwa Tanu haina dosari wataingiza ulaghai, uchochezi na fitina ili watimize shabaha zao za kishetani. Naiomba Serikali ya kibeberu itamke wazi kuwa inaishambulia Tanu kwa sababu tumetangaza wazi bila woga kuwa serikali ya mabavu tutaipiga vita. Tutaishambulia bila kupumua mpaka tumeiangusha. Hatutashika silaha, hatutatumia udanganyifu. Tutazitumia njia hizi kama vile tunavyotangaza nia yetu. Hatutavumilia kuonewa.”
Baada ya kuchapishwa makala hayo, Nyerere alikamatwa, akashtakiwa. Hiyo ni kwa mujibu wa mwandishi Kiluba Nkulu katika kitabu chake, ‘Serving the Common Good: A Postcolonial African Perspective on Higher Education.’
Katika kitabu cha ‘kesi ya Julius Kambarage Nyerere,’ mwandishi Simon Ngh’waya anaandika “baada ya wiki moja kupita, Serikali iliamua kuanzisha kesi ya kashfa dhidi ya Nyerere... Tarehe 5 Juni, 1958 saa 10:30 jioni, makao makuu madogo ya sasa ya chama, barabara ya Lumumba, Dar es Salaam, ... yalivamiwa na askari polisi wa Idara ya Upelelezi wakiongozwa na kaimu kamishna wa polisi aliyejulikana kwa jina la M. T. Mackinley.”
Nyerere alifikishwa mahakamani Jumatatu ya Juni 9, 1958 akikabiliwa na mashtaka matatu ya kashfa katika kesi namba 2207/58. Kesi hiyo ilianza kusikilizwa Jumatano ya Julai 9, 1958.
Hakimu aliyeisikiliza kesi hiyo ni L.A. Davies. Mwanasheria wa Serikali na kiongozi wa mashtaka alikuwa J.vC. Summerfield. Wanasheria waliomtetea Nyerere ni Mahamoud Rattansey na Kantilal L. Jhaveri. Nyerere alisimama kizimbani kwa makosa ya kuwakashifu DC Weeks wa Musoma na DC Scott wa Songea.
Alipoanza kutoa ushahidi Agosti 11, 1958, Nyerere alikiri ndiye aliyechapisha makala hayo na aliyeandika akiwa na shabaha ya kuitaka Serikali itupie macho malalamiko ya watu.
“Sikutaka kuyaandika malalamiko hayo mapema hadi nilipogutushwa na kitendo cha Serikali kuyafunga matawi ya Tanu Geita,” alisema Nyerere.
Mahakama ilipokutana tena Jumatano ya Julai 16, 1958 upande wa mashtaka uliamua kufuta shtaka la kwanza dhidi ya mshtakiwa Nyerere. Kadhalika upande wa mashtaka uliamua kulifanyia marekebisho shtaka la pili lililokuwa linamkabili. Hukumu ya kesi hiyo ilitolewa Jumatano ya Agosti 13, 1958. Nyerere alitiwa hatiani. Sehemu ya hukumu ya Hakimu Davies inasema “Nyerere hakuwa na haki kisheria, kwa njia yoyote ile, wala kuwajibika kijamii alipoamua kuandika maneno hayo ya kashfa hadharani! Haukutolewa ushahidi wowote mbele yangu kuthibitisha kwamba Nyerere alichukua jukumu lolote kupeleleza madai dhidi ya Scott. Nyerere alikiri katika ushahidi wake kwamba alifahamu kuwa Scott hakufunga tawi la Tanu. Lakini alikuwa akitekeleza sheria alipokataa kuliandikisha tawi hilo la Tanu. Kwa hiyo, Nyerere hakufanya hivyo kwa nia njema.
“Isipokuwa aliandika maneno hayo ya kashfa kwa sababu anazozifahamu mwenyewe, siwezi kuridhika na maneno yake kwamba maneno aliyoyaandika yalikuwa ya kweli, hasa ikizingatiwa kwamba hakuwa na upendeleo wa aina yoyote kuandika maneno hayo.” Hakimu alimaliza kusoma hukumu yake na akasema Nyerere ana hatia kama alivyoshitakiwa. Baada ya maoni ya kisheria na ilipoonekana hilo ni kosa la kwanza la Nyerere, Hakimu Davis akatoa adhabu. Akasema “namtoza mshtakiwa faini ya Sh3,000 au jela miezi sita. Nampa mshtakiwa siku mbili kulipa faini hiyo.” Nyerere alilipa faini na kuachiwa huru.
Ingawa Nyerere alipewa nafasi ya kulipa faini na hivyo kuachiwa huru, si wote walikuwa na bahati kama yeye kwenye kesi hizo za uchochezi zilizofunguliwa na Serikali ya kikoloni.
Mhariri jela kwa uchochezi
Yote hayo yalianza mwaka 1955 wakati Baraza la Kutunga Sheria la kikoloni lilipopitisha sheria waliyoiita ‘Incitement to Violence Act’ ambayo kwa kukosoa tu watu wa rangi nyingine kungetosha kukufungulia mashtaka ya uchochezi na mzigo wa kuthibitisha kuwa hukutenda kosa hilo.
Mhariri wa gazeti la ‘Mwafrika’ hakupata bahati aliyoipata Nyerere. Gazeti hilo lililokuwa linatoka mara mbili kwa juma, lilikuwa linahaririwa na Robert Moses Makange, ambaye awali alikuwa katibu mkuu msaidizi wa Tanu na mjumbe wa kamati kuu ya Tanu, lilitolewa mara ya kwanza mwaka 1957 kama gazeti la kwanza la kisiasa lililochapishwa na Waafrika.
Makange alikuwa mwandishi na mhariri tangu lilipoanzishwa mwaka 1957 hadi 1961. Ukiondoa muda aliotumikia kifungo gerezani. Gazeti hilo lilifanya kazi kubwa ya kueneza siasa ya Tanu ya kudai uhuru. Katika toleo namba 19 la Jumapili ya Juni Mosi, 1958, gazeti hili liliandika hivi:
“Sisi wote tunajua kuwa Mwingereza yupo hapa kwetu kwa sababu ya kutunyonya damu na kujipatia manufaa yake mwenyewe, na wala asitudanganye kwamba yupo hapa kwa kuwa anatuonea huruma na kutaka kutufundisha ustaarabu au kuleta maendeleo ya nchi. Maneno haya ni kigeugeu cha kutaka kutufunika macho; na kwa kadri atakavyozidi kuwa hapa ndivyo madini na fedha zitakavyozidi kutolewa katika nchi hii kupelekwa kwao, ambako bila ya sisi hawawezi kuishi sawasawa.”
Baada ya habari hiyo, Makange na mchapishaji wake, Kheri Rashidi Baghelleh walikamatwa na kushtakiwa kwa uchochezi. Kutokana na sheria ya kikoloni iliyotajwa hapo juu iliyotungwa miaka mitatu kabla, Makange na Baghelleh walishindwa kesi hiyo. Hata baada ya kukata rufaa walishindwa pia.
Hatimaye walifungwa miezi sita na Serikali ya mkoloni kwa tuhuma za uchochezi uliodaiwa kuwa ungeweza kusababisha vurugu za ubaguzi wa rangi.
Pamoja na kwamba walihukumiwa kwenda gerezani, gazeti hilo halikupigwa marufuku, pengine kwa hofu ya watawala kwamba hali ingekuwa mbaya zaidi. ‘Mwafrika’ likampata mhariri mpya, Joel Mgogo.
Walipotoka gerezani Desemba 1958 walipata mapokezi makubwa kutoka kwa vijana wa Tanu waliojipanga barabarani kuanzia gereza walilokuwa wamefungwa hadi yaliko makao makuu ya chama Mtaa wa Lumumba.
Mwaka uliofuata, 1959, chama cha Tanu kiliacha kulifadhili gazeti hilo na badala yake kikaanzisha gazeti mbadala lililoitwa ‘Ngurumo’ ambalo lilichapishwa mara ya kwanza Jumatano ya Aprili 15, 1959 kama gazeti la kila siku.

MIAKA 20 BILA NYERERE: Nyerere ateua baraza la kwanza la mawaziri


Baada ya Tanu kupata tena viti vingi katika uchaguzi wa 1960, Gavana Richard Turnbull alimwambia Mwalimu Nyerere aunde serikali. Mkutano wa Katiba ulifanyika mjini London, Machi 1961.
Hatimaye Tanganyika ikapata serikali ya kujitawala Jumatatu ya Mei 1, 1961 ingawa bado gavana alikuwa na mamlaka fulani katika mambo muhimu ya nchi. Hata hivyo Nyerere akawa waziri mkuu wa kwanza na baraza lake la mawaziri likawa kama ifuatavyo:
Rashidi Mfaume Kawawa:
Aliteuliwa waziri asiye na wizara maalumu kabla hajawa Waziri wa Serikali za Mitaa. Baada ya Nyerere kujiuzulu uwaziri mkuu, 1962, alimteua Kawawa kuwa waziri mkuu na kudumu na wadhifa huo hadi Desemba 9, 1962 Tanganyika ilipokuwa Jamhuri. Agosti 1958 alichaguliwa kuingia Baraza la Kutunga Sheria na baadaye aliteuliwa kuwa Waziri wa Serikali za Mitaa na Nyumba. Alizaliwa Songea Alhamisi ya Mei 27, 1926. Alifariki Desemba 31, 2009 akiwa na miaka 83.
Abdallah Said Fundikira:
Aliteuliwa Waziri wa Ardhi, Upimaji Ramani na Maji. Huyu alikuwa Mtemi wa 19 wa Unyanyembe. Utawala wake ulidumu miaka mitano tu 1957-1962. Nyerere alifuta utemi wa dola rasmi mwaka 1962. Hata hivyo, baada ya utemi kufutwa, aliteuliwa kuwa waziri. Alizaliwa Februari 2, 1921 huko Unyanyembe. Alifariki Agosti 6, 2007, akiwa na miaka 86.
Sir Ernest Vasey:
Aliteuliwa Waziri wa Fedha, hakuwa Mtanganyika. Aliingia Afrika Mashariki mwaka 1936 na kukaa Kenya miaka 23 huku akishika nyadhifa mbalimbali ikiwamo mbunge wa kuchaguliwa wa Nairobi Kaskazini. Mwaka 1952 aliteuliwa kuwa Waziri wa Fedha na Maendeleo wa Kenya hadi 1959. Alipoingia Tanganyika, Februari 1960, akateuliwa Waziri wa Fedha wa Tanganyika. Sir Vasey aliteuliwa na Gavana, kwa maombi ya Mwalimu Nyerere, kuingia Legico, kabla ya Nyerere kumteua kuwa waziri. Alisoma bajeti yake ya kwanza mwaka wa fedha wa 1960/61, Aprili 7. Nyerere alipojiuzulu uwaziri mkuu, Sir Vasey naye alijiuzulu nafasi yake. Alizaliwa 1901, Uingereza. Alifariki 1984 akiwa na miaka 83.
Amir Habib Jamal:
Alikuwa Waziri wa Viwanda. Ni Mhindi pekee aliyekuwa katika serikali ya kwanza ya Tanganyika na ambaye aliendelea kuwapo baada ya uhuru. Juni 1959 aliingia serikalini mara ya kwanza alipoteuliwa kuwa Waziri wa Tawala za Miji na Majengo katika serikali ya muda ya Tanganyika. Uteuzi huo ulitokana na uchaguzi wa kura tatu mwaka 1958. Jamal, mwenye asili ya India, alizaliwa Januari 26, 1922 nchini Tanganyika na alifariki Machi 21, 1995 akiwa na miaka 73.
Asanterabi Zephaniah Nsilo Swai:
Aliteuliwa Waziri wa Biashara. Kabla ya hapo alikuwa meneja mkuu Chama cha Ushirika Meru na alikuwa mwenyekiti wa Tanu mkoa wa Kanda ya Kaskazini. Alikuwa pia mwenyekiti kamati ya uchumi na ustawi wa jamii ya Tanu. Alipata elimu vyuo vikuu vya Makerere, Uganda; Bombay, India na Pittsburg, Marekani na Chuo Kikuu cha Delhi, India. Alizaliwa Aprili 20, 1925 Moshi, Kilimanjaro na kufariki Januari Mosi, 1994 akiwa na miaka 69.
Tewa Said Tewa:
Aliteuliwa kuwa Waziri wa Ardhi na Upimaji. Alizaliwa mwaka 1924 jijini Dar es Salaam, alikuwa akiishi Magomeni Mikumi na mmoja wa watu wa mwanzo kumpokea na kufahamiana na Nyerere alipokuja Dar es Salaam mwaka 1952. Tewa ni kati ya wale wazalendo 17 walioasisi Tanu. Alifariki mwaka 1998 akiwa na miaka 74.
Paul Lazaro Bomani:
Alikuwa Waziri wa Ukulima na Maendeleo ya Ushirika. Mzaliwa wa Ikizu, Musoma, aliingia katika serikali ya Nyerere akiwa na miaka 35. Kama Kahama. Bomani naye alijishughulisha sana na ushirika katika Kanda ya Ziwa na alikuwa kiongozi wa chama cha Ushirika cha Victoria Federation of Co-operative Unions (VFCU). Alipata elimu ya ushirika Chuo cha Loughborough, Uingereza. Mwaka 1958 alipita bila kupingwa kuwa mjumbe wa Legico. Alizaliwa Januari Mosi, 1925. Alifariki Aprili Mosi, 2005 akiwa na miaka 80.
Oscar Salathiel Kambona:
Aliteuliwa kuwa Waziri wa Elimu akiwa na miaka 32. Kambona, alikuwa mtoto wa kasisi na alipata elimu yake shule za Alliance zilizokuwa Dodoma na Tabora. Alisoma sheria Chuo Kikuu cha Middle Temple, London, Uingereza na wakati anateuliwa kuingia Baraza la Mawaziri alikuwa Katibu Mkuu wa Tanu. Alizaliwa Agosti 13, 1928, Kwambe karibu na Mbamba Bay. Alifariki mjini London Julai 1997 akiwa na miaka 69.
Derek Noel Maclean Bryceson:
Alikuwa mkulima, lakini aliteuliwa Waziri wa Afya na Masuala ya Wafanyakazi akiwa na miaka 37. Bryceson aliingia Tanganyika mara ya kwanza mwaka 1952 akitokea Kenya. Alisoma Chuo Kikuu cha Cambridge, Uingereza na alikuwa katika kikosi cha Jeshi la Anga la Uingereza wakati wa Vita Kuu, II ya Dunia. Mara ya kwanza aliingia serikalini mwaka 1957 kwa cheo cha Waziri Msaidizi wa Kazi za Starehe, na baadaye, Juni 1959, akawa Waziri wa Machimbo ya Madini na Biashara, na mwaka uliofuata, 1960, akaingia katika Serikali ya Mwalimu Nyerere. Tofauti na Wazungu wenzake waliokuwa katika serikali ya Nyerere, Bryceson alikuwa mjumbe wa kuchaguliwa wa Legico wa Jimbo la Kaskazini. Bryceson ni raia wa Uingereza aliyezaliwa China, Desemba 31, 1922. Alifariki, Oktoba 1980 akiwa na miaka 58
Clement George Kahama:
Aliteuliwa kuwa Waziri wa Usalama na Amani ya Nchi (Waziri wa Mambo ya Ndani). Kahama kutoka Karagwe, aliteuliwa uwaziri akiwa na miaka 32. Alipata elimu Sekondari ya Tabora na Chuo cha Loughborough, Uingereza. Alikuwa mtunza hazina chama cha wakulima cha Bukoba (BCU) na kiongozi mkuu wa kwanza wa ushirika huo mwaka 1956. Alijishughulisha sana na halmashauri ya mji wa Bukoba na halmashauri ya Buhaya na aliingia Legico kutoka Jimbo la Ziwa Magharibi katika uchaguzi mkuu wa mwaka 1958. Alizaliwa Karagwe Novemba 30, 1929. Alifariki jijini Dar es Salaam, Machi 12, 2017 akiwa na miaka 88.
Job Malecela Lusinde:
Aliteuliwa Waziri wa Serikali za Mitaa. Alijiunga na Tanu mwaka 1955 baada ya kurejea kutoka masomoni Makerere, Uganda. Katika Jimbo la Kati, Lusinde alikuwa naibu katibu wa Tanu wa jimbo. Mwaka 1959 alikuwa ofisa mtendaji halmashauri ya wilaya ya Dodoma kabla ya kuwa mwenyekiti wa halmashauri ya mji huo mwaka 1960. Alizaliwa Oktoba 9, 1930 mkoani Dodoma.
Baada ya Tanganyika kuwa Jamhuri, Nyerere alifanya mabadiliko kidogo ya Baraza la Mawaziri. Alifuta cheo cha waziri mkuu na kuunda cha Makamu wa Rais kama Katiba ilivyotaka. Na Kawawa akawa Makamu wa Rais.
Katika mabadiliko hayo, Chifu Abdallah Fundikira aliteuliwa kuwa Waziri wa Sheria lakini alijiuzulu mwaka uliofuata yaani 1963, baada ya kutuhumiwa kwa rushwa.
Kambona alichukua uwaziri wa Mambo ya Ndani kutoka kwa George Kahama. Katika mabadiliko ya mwaka 1963, Kambona akawa Waziri wa Mambo ya Nje na Ulinzi. Kabla ya mwaka 1963 wizara hiyo ilikuwa chini ya Rais Nyerere. Kahama akawa Waziri wa Biashara. Bomani akachukua uwaziri wa Fedha kutoka kwa Ernest Vasey.
Nyerere akaongeza na mawaziri wengine. Hao ni pamoja na Sheikh Amri Abeid, Jeremiah Kasambala, Saidi Ali Maswanya, Michael Kamaliza, Austin Shaba, Lawi Nangwanda Sijaona na Solomon Eliufoo.
Kutokana na hilo, baraza jipya la mwaka 1963 likawa na Sheikh Amri Abeid (Waziri wa Sheria), Bryceson (Kilimo), Kahama (Biashara), Kambona (Mambo ya Nje na Ulinzi) na Lusinde (Mambo ya Ndani).
Wengine ni Jamal (Mawasiliano), Bomani (Fedha), Tewa (Ardhi), Kasambala (Ushirika na Maendeleo ya Jamii), Eliufoo (Elimu), Maswanya (Afya) na Kamaliza (Kazi).
Pia walikuwapo Shaba (Serikali za Mitaa), Sijaona (Mila na Utamaduni), Swai (Mipango ya Maendeleo). Nafasi ya uwaziri mkuu ilirejeshwa Februari 1972 alipoteuliwa Kawawa hadi mwaka 1977 alipoteuliwa Edward Moringe Sokoine.

Post a Comment

0 Comments