MIAKA 20 BILA YA NYERERE: Wahaini wa 1968 walivyoadhibiwa-4

  Oscar kambona


Ingawa alikuwa maarufu sana Tanzania, Afrika na duniani kwa ujumla, Mwalimu Julius Nyerere alikabiliana na magumu mengi katika siasa. Alikuwa katika majaribio mengi ya utawala wake kuangushwa. Wengi waliomwinda walikuwa ni wa ndani na nje ya serikali yake. Kulikuwa pia na majaribio mengi ya kuidhoofisha serikali yake.
Nyerere alikabiliana na mataifa ya Magharibi, makaburu wa Afrika Kusini na pia Wareno. Lakini jaribio lililoonekana kuwa kubwa zaidi lilifanywa na Watanzania wenyewe-jaribio la kuipindua serikali yake.
Ingawa kulikuwa na uhaini wa mwaka 1982 kulipokuwa na njama za kuipindua serikali yake ambapo askari 600 walikamatwa na kiasi cha raia 1,000 kutiwa nguvuni Januari 1983 wakidaiwa kushiriki njama za uhaini, hakuna tukio la uhaini lililosikika kama lile la Oktoba 1969.
Ilidaiwa kuwa uhaini huo ulipangwa na Oscar Kambona akishirikiana na maofisa wakubwa wa serikali. Kambona alikuwa ameikimbia nchi tangu Julai 1967, miezi takriban mitano baada ya Azimio la Arusha.
Mashtaka yaliletwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mark Bomani, na baadaye mwanasheria wa Serikali, Nathaniel King.
Pamoja na Oscar Kambona, waziri wa zamani wa Mambo ya Nje na Ulinzi wa Tanganyika, ambaye mwaka 1967 alikimbilia uhamishoni Uingereza mara baada ya kutangazwa kwa Azimio la Arusha, walihusishwa watu wengine waliodaiwa kula njama za kuiangusha serikali ya Mwalimu Nyerere wakiongozwa na Kambona. Kesi yao ilianza Jumatatu ya Juni 8, 1970 katika Mahakama Kuu ya Tanzania mbele ya Jaji Mkuu, Philip Telford Georges.
Bila kutambua kilichokuwa kinatokea, watu saba: Gray Likungu Mattaka, John Dunstan Lifa Chipaka, Bibi Titi Mohamed, Michael Marshall Mowbray Kamaliza, Eliyah Dunstan Lifa Chipaka, William Makori Chacha na Alfred Philip Milinga walijikuta wakifikishwa mahakamani kwa kosa la uhaini, wakituhumiwa kula njama za kuiangusha Serikali ya Tanzania na kupanga nyama za kumuua Rais wake, Mwalimu Julius Nyerere.
Gray Likungu Mattaka (34) zamani alikuwa mhariri wa habari wa katika gazeti la chama cha Tanu, The Nationalist na Uhuru. Mattaka alijulikana pia kwa majina mengine ambayo ni Chaima, Kavuma, Mikaya au Edward Kavuma.
John Dunstun Lifa Chipaka (38) alikuwa katibu wa zamani wa chama cha Congress. John Chipaka kwa mujibu wa hati za mashitaka, alikuwa na majina mengine ya bandia kama M. M. Chimwala, Chimwala Ching—wechene, Chimwala au Padre John Chimwala.
Bibi Titi Mohamed (45) ni rais wa zamani wa Umoja wa Wanawake wa Tanzania (UWT). Inasemekana naye alikuwa na majina mengine aliyojiita au kuitwa. Hayo ni pamoja na Mama Mkuu, Mwamba au Anti.
Michael Marshall Mowbray Kamaliza (40) alikuwa Katibu Mkuu wa zamani wa Nuta (Chama cha Wafanyakazi nchini) na kadhalika waziri wa zamani wa kazi na alikuwa na majina mengine ya bandia kama Palijekantu, Bwana Miguu, Wamaliza au Hakuna Kitu.
Eliya Dunstan Chipaka (32) ni ndugu yake John Chipaka. Eliya Chipaka alikuwa ofisa wa zamani katika jeshi. William Makori Chacha (46) alikuwa kanali wa jeshi na majina mengine ya bandia aliyotumia ni pamoja na Ben Tasu au Kitumbo.
Kisha kuna Alfred Philip Milinga (27) aliyekuwa ofisa wa zamani wa jeshi. Oscar Selathie Kambona, alitoroka Tanzania na kwenda kuishi Uingereza.
Kesi hiyo iliyoanza kusikilizwa kuanzia Jumatatu ya Juni 8, 1970 ilidumu kwa siku 127. Hiyo ilikuwa ni kesi iliyosikilizwa kwa muda mrefu zaidi katika historia ya Tanganyika na Tanzania kufikia wakati huo. Jaji Georges hakuwahukumu watuhumiwa hao adhabu ya kifo kama sheria iliyokuwa inaelekeza, lakini alimhukumu kila mmoja na hukumu yake.
Bibi Titi Mohamed, Gray Likungu Mataka, Elia Dunstan Lifa Chipaka na John Lifa Chipaka walihukumiwa vifungo vya maisha gerezani. Michael Kamaliza na William Makori Chacha walihukumiwa kifungo cha miaka kumi kila mmoja.
Alfred Philip Milinga alifutiwa mashtaka yote, lakini hiyo ni baada ya kuwekwa kizuizini kwa miezi 16 chini ya Sheria ya Kizuizini wakati upelelezi wa kesi hiyo ulipokuwa unaendelea.
Sheria hiyo ilipitishwa na Bunge kuiruhusu Serikali kuwakamata watu na kuwaweka kizuizini kama walidhaniwa kuhatarisha usalama wa taifa lakini ililalamikiwa na Jaji Mkuu wakati kesi hiyo ya uhaini ikiendelea.
Jaji Georges alilaumu kuwa sheria hiyo ilikuwa mbaya kwa sababu iliruhusu watu kushikiliwa kwa muda mrefu bila kufikishwa mahakamani.
Kambona, ambaye alitajwa kuwa ni kiongozi wa uhaini huo, alihukumiwa bila yeye kuwapo mahakamani.
Hata hivyo, miaka saba baada ya hukumu ya kesi hiyo, Bibi Titi Mohamed aliachiwa huru kwa msamaha wa Rais Nyerere. Kitabu ‘Historical Dictionary of Women in Sub-Saharan Africa’ cha Kathleen E. Sheldon (uk. 155) kinasema Bibi Titi aliachiwa huru mwaka 1972.
Kitabu ‘Nyerere and Africa: End of an Era’ cha Godfrey Mwakikagile (uk. 373) kinasema walioachiwa pamoja na Bibi Titi mwaka 1972 ni pamoja na Eli Anangisye, ambaye awali alikuwa Katibu Mkuu wa umoja wa vijana wa Tanu (Tanu Youth League) ambaye naye alikuwa amewekwa kizuizini akituhumiwa kuhusika na njama nyingine za kuipindua serikali ya Nyerere.
Mwaka 1977 alitoka gerezani mkoani Dodoma baada ya kudaiwa kuwa alimwandikia Rais barua ya kumwomba msamaha kwa yote aliyotenda.
Februari 5, 1978, Otini Kambona, ambaye ni ndugu yake Oscar Kambona na ambaye awali alikuwa Waziri wa Elimu na Habari, pamoja na Mattiya Kambona, waliachiwa huru kutoka gerezani pamoja na wengine 22 waliokuwa wametiwa kizuizini. Pia siku hiyo waliachiwa huru wafungwa wengine 7,000 kwa msamaha wa Rais.
Wote hawa waliachiwa huru katika maadhimisho ya kwanza ya kuzaliwa kwa CCM na miaka 11 ya Azimio la Arusha. Otini na Mattiya hawakufikishwa mahakamani na kwa sababu hiyo hawakuhukumiwa, bali walikuwa wamewekwa kizuizini ambako walikaa kwa miaka 10 tangu Desemba 1967 kwa sababu walikuwa wakimuunga mkono kaka yao, Oscar Kambona, na kwa kutumia gazeti alilomiliki la ‘Ulimwengu’ kuendesha propaganda za kisiasa.
Gazeti hilo lilikuwa likichapisha pia makala zilizoandikwa na Oscar Kambona akiwa uhamishoni Uingereza. Kambona mwenyewe hakuwahi kukamatwa, na wala hakukuwahi kufanyika jitihada zozote za kumrejesha nchini ili ashtakiwe pamoja na wale aliotuhumiwa kula nao njama.
Aliendelea kukaa nchini Uingereza hadi aliporejea nchini kwa hiari yake mwenyewe mwaka 1992 ulipoanzishwa mfumo wa vyama vingi vya siasa.

MIAKA 20 BILA NYERERE: Hotuba ya Mwalimu Nyerere, Kuzungumza uzanzibari si fahari



Tuliijenga nchi mpya. Imara. Ni imara tu, na uimara wake ulikuwa unasifiwasifiwa sana. Lakini imetikiswa. Na nyufa tumeziona. Imetikiswa na nyufa tumeziona. Nyingine katika paa, nyingine katika dari, nyingine kutani na nyingine katika misingi.
Tunachotaka ni kwamba mtikisiko usiendelee. Tuchomee. Tuichomee iwe imara zaidi. Kwa hiyo matumaini ni kwamba tunaona hivyo wote tunaona hivyo, nchi yetu imetikiswa. Nitaeleza zile nyufa mimi ninazoziona. Nitazieleza baadaye.
Tunachotaka ni kwamba nyufa hizo zieleweke na tukubaliane kwamba kazi yetu ni kuziziba. Na tupate uongozi unaoelewa hivyo, kwamba kazi ni kuziba nyufa tulizoziona katika taifa letu. Kazi si kuendelea kulitikisa taifa. Litabomoka. Halitabaki. Sasa nyufa gani hizo. Ya kwanza mliniambia Muungano Mwalimu. Ufa wa kwanza ni Muungano. Wote mnajua. Mnaniambia ‘Mwalimu Muungano sasa ni imara zaidi kuliko miaka ishirini iliyopita?’
Ilipotikisika ufa mmoja mkubwa tuliouona ni katika Muungano. Watu wazima wameuzungumza Muungano, kama tuuvunje au uendelee. Ilikuweko hatari ya kuvunjika kwa Muungano, wala haijesha.
Watu wamezungumza Uzanzibari. Baadhi ni viongozi wetu. Wanajivunia Uzanzibari. Nadhani wengine wanafikiria hata kujitenga. Wapo, si wengi, lakini wapo.
Kujitenga maana yake ni kuvunja nchi. Ivunjike. Tusiwe na nchi moja tuwe na nchi mbili. Ni jambo linazungumzwa. Tunataka kiongozi na viongozi watakaoelewa hivyo.
Huu, kuzungumza Uzanzibari si fahari. Si jambo la fahari. Hatima yake mtavunja nchi. Zanzibari. Mtu mwenye akili hawezi kufikiri Mzanzibari hana akili. Hawezi akautukuza Uzanzibari kwa kujiita sisi Wazanzibari na wao Watanganyika. Sisi Wazanzibari na wao Watanganyika.
Nadhani ile ina usalama ndani yake. Kwamba Uzanzibari ule na Utanganyika ule una usalama ndani yake. Hatima yake Zanzibar itajitenga.
Zanzibar ikijitenga kutokana na ulevi tu, ‘sisi Wazanzibari wao Watanganyika’, ulevi tu, ulevi hasa ulevi wa madaraka. Ikitokea hivyo kwamba ‘sisi Wazanzibari na wao Watanganyika’, wakumbuke kwamba Muungano ndio unaowafanya wanasema sisi Wazanzibari wao Watanganyika.
Nje ya Muungano hawawezi kusema hivyo. Nje ya Muungano hakuna Wazanzibari. Nje ya Muungano kuna wao Wapemba sisi Waunguja (vifijo). Nataka mjue hivyo. Nataka mjue hivyo. Nje ya Muungano hakuna sisi Wazanzibari wao Watanganyika. Hakuna.
Kinachowafanya sasa wajiite sisi ni ubaguzi wa kuwabagua Watanganyika. Wakiishakuwabagua Watanganyika, ile dhambi ya ubaguzi haifi, inaendelea. Dhambi ya ubaguzi ukishakuitenda inaendelea ni sawasawa na kula nyama ya mtu. Ukila nyama ya mtu utaendelea tu kuila.
Mtamaliza, mtatengana na Watanganyika halafu mara mtakuta kumbe sisi si Wazanzibari. Kuna Wapemba kuna Waunguja. Mtakuta hivyo.
Wapemba watapata msukosuko kidogo aah ooh! Mtakuta kumbe kuna Wazanzibari na Wazanzibara. Hamtakaa salama. Hamwezi kukaa salama baada ya kutenda dhambi ya kubagua watu wa nchi yenu ile ile moja. Mkawaita wale wao na hawa sisi.
Dhambi ile haiishii hapo. Ndivyo historia ilivyo. Ni sheria ya historia si sheria ya Mwalimu Nyerere. Huwezi kufanya ubaguzi wa namna hiyo halafu dhambi ile ikuache hapo hapo, hapana. Itakuandama.
Namalizia hilo hapo. Ninalolisema kwa Wazanzibari nalisema kwa Watanganyika. Zanzibar wanaweza wakajitenga. Wanaweza wakajitenga hivi kwa ujinga, kwa ulevi, kwa ujinga hata kwa ujinga wa viongozi wao wanaweza kujitenga. Wanaweza wakajitenga hivi.
Na Watanganyika wakabaki wameduwaa tu. ‘Loh Wazanzibari hawa wamefanyaje. Wanatuacha wenzetu hawa wanatuacha jamani. Wanakwenda zao wenzetu’.
Wakawaacha Watanganyika wameduwaa. Watanganyika walioachwa wameduwaa kwa kitendo cha Wazanzibari kuwakimbia watabaki wamoja. Hawataparaganyika. Narudia. Wazanzibari wanaweza wakatoka. Wakajitenga wenyewe tu. ‘Sasa wengine wana bendera sisi hatuna bendera kwa nini wengine wana wimbo wa taifa sisi hatuna, kwa nini,’ basi … si wote wanaosema hivyo, ni viongozi wanaosema hivyo. Basi, halafu wakajitenga. Wakawaacha Watanganyika wameduwaa.
Wakiwaacha Watanganyika walio katika hali hiyo, Watanganyika wanaowashangaa Wazanzibari katika kuwaacha, Watanganyika hao watakuwa salama. Watakuwa salama. Watanganyika wakiwakataa Wazanzibari, kwa tendo la dhambi ile ile, ‘sisi Watanganyika, wao Wazanzibari’. Wakautukuza usisi Tanganyika. Na kwa hiyo wakawafukuza Wazanzibari. Hawabaki salama. Hapatakuwa na Tanganyika.
Wakishakujitenga tu Wazanzibari wale. Wakishakujitenga tu Wazanzibari. Wako kando hivi. Mmewafukuza. Mmejidai wakubwa nyinyi … mkawatimua. Mkapata Yeltsin wenu hapa akawatimua. Hambaki.
Kwani mtasema je. Mtakuwa mmeshasema sababu ya kuwafanya wale wao na ninyi ni ninyi, wao vipi… Halafu mbaki ninyi. Maana wako watakaosema Wazanzibari tu, Wazanzibari kana kwamba kuna kabila lao Wazanzibari. Mmewabagua.
Mtaanza nyumba za Wapemba mtaziingilia pale sasa hivi. Viko vijumba vijumba vya Wapemba huku. Waliwahi kukimbia baadhi yao walikimbia wakati uleee zamani.
Vijumba vya kwanza vitapitia ‘Wapemba, Wapemba’. Mtamaliza vya Wapemba. Halafu mtakuta ninyi mliokuwa mnajiita sisi Watanganyika mtakapoanza kuchoma nyumba za Wapemba mnazichoma moto zile, mtakuta ah! Si sisi.
Sisi hawa wote si wamoja. Mbona za Wapemba tunachoma za Wachaga hatuchomi kwa nini. Maana Wachaga si wazawa bwana. Hapa kuna wazawa sasa unachoma za Wachaga tu?
Mtakuta hakuna watu wanaitwa Watanganyika. Mtakuta mlijidanganya tu mnadhani kuna watu wanaitwa Watanganyika. Hakuna. Kuna Wagogo kuna Wanyamwezi kuna Wasukuma kuna Wazanaki kuna Wakurya kuna Wamwera …eh! Wengi sana. Siwezi kuwataja wote.
Mtakuta hakuna kitu kizima hivi kinaitwa sisi Watanganyika. Na madhali mmefanya dhambi ya kusema wao Wazanzibari si wenzetu dhambi ile ile itawatafuna ninyi.
Na mimi nasema Mwenyezi Mungu anisamehe, mnastahili iwatafune. Hamwezi kutenda dhambi kubwa namna ile bila adhabu. Na adhabu zingine zimo mle mle ndani ya kitendo. Hazisubiri.
Hilo la kwanza. Kwa hiyo, la kwanza ninalosema tunao ufa wa Muungano. Ufa wa kwanza kabisa mkubwa kabisa …Tunataka Rais Mtanzania.
Rais tunayemtaka ni Mtanzania. Hatuwezi kupata Rais Mtanzania asitoke ama Zanzibar ama Tanganyika. Atatoka ama Zanzibar ama Watanganyika.
Lakini hatumchagui kwa sababu ya Uzanzibari wake. Hatumchagui kwa sababu ya Utanganyika wake. Na akiuweka mbele Uzanzibari wake akauweka mbele Utanganyika wake, tunajua huyu hatufai.
Hiyo ndiyo sifa mama. Kwa sababu tunayemtaka ni Rais wa Tanzania. Mimi niko hapa kuzungumza habari ya Rais wa Tanzania. Mimi nilikuwa wa kwanza, tunaye wa pili, na sasa namsemea wa tatu. Tunataka Rais wa Tanzania. Hiyo ndiyo sifa yake ya kwanza. Ndiyo sifa mama. Hana hiyo hatumtaki hata angekuwa na sifa nyingine zote. Atavuja nchi yetu. Hatufai. Ya kwanza.
Ya pili inafanana kidogo na hiyo. Inafanana kidogo na hiyo. Rais wa nchi yetu anachaguliwa kutokana na Katiba ya Tanzania. Na akiishakuchaguliwa anaapishwa.
Kama ni Mkristu, kwa Biblia. Kama ni Mwislamu kwa Kuruani. Hatuchagui mtu asiyemwamini Mungu. Lakini tukimchagua tutatafuta utaratibu wa kumwapisha. Ataapa. Hata asiyekuwa muumini tutamwapisha kwamba atailinda na kuitetea Katiba ya Tanzania. Asipoilinda tunamjua ni msaliti. Tutamwapisha. Ataapa. Lazima kabisa. Hata kama si muumini. Na kwa mujibu wa Katiba yetu si lazima mtu awe mwamini Mungu kuwa Rais. Hata kidogo.
Lakini tutamwapisha. Umechaguliwa kwa mujibu wa Katiba ya nchi yetu. Unaapa kuilinda. Ataapa kwa huyo Mungu wake au akili yake anayoijua lakini atatuapia. Ataapa kusudi tuweze kumshitaki, tuweze kumshitaki kama akikiuka.
Itaendelea kesho...

Post a Comment

0 Comments