Nitakumbushia hapa, tukio la utekaji wa ndege ya abiria ya Ufaransa iliyokuwa na abiria wengi wa Kiyahudi. Na mmoja wa wahusika wakuu katika tukio hili la kigaidi alikuwa Jenerali Idd Amin Dadah wa Uganda.

Ndio, licha ya Jenerali Idd Amin kuendesha ugaidi wa dola kwa
maana ya State Terrorism, kwenye tukio hili, Jenerali Idd Amin
alishiriki rasmi kwenye Ugaidi wa Kimataifa. Maana, tukio lile la
utekaji ndege lilianzia Ulaya, likaambaa Mashariki ya Kati na
kumalizikia kwenye ardhi ya Uganda. Ni kwenye uwanja wa ndege wa Entebbe huku Idd Amin mwenyewe akishiriki kuratibu harakati za
kigaidi.

Maelezo marefu juu ya sakata ya Entebbe yanasimuliwa kwa umahiri mkubwa na mwandishi William Stevensson katika kitabu chake cha (90 Minutes At Entebbe), Yaani Dakika 90 katika Entebbe.

Ndege hiyo ilitekwa nyara Juni 27, 1976 mara ilipoanza kuruka
kutoka uwanja wa ndege wa Athens nchini Ugiriki kuelekea Tel Aviv. Miongoni mwa watekaji nyara, walikuwemo Wapalestina, lakini raia mmoja wa Ujerumani naye alishiriki utekaji huo. Mjerumani huyo alikuwa ni mfuasi wa kikundi cha kigaidi cha Ujerumani kulichojulikana kama ”Baader-Meinhof.”

Inasadikiwa, kuwa Dr. Wadi Hadad, mwanaharakati na Kiongozi wa chama cha ukombozi wa Wapalestina cha PFLP (Popular front For Liberation of Palestene) alishiriki kwenye kupanga kazi hii ya kigaidi. Bila shaka, inaaminiwa pia, kuwa aliyekuwa gaidi nambari moja wakati huo, Ramirez Carlos, ambaye pia alijulikana kama ”The Jackal”, alikuwa na mkono wake kwenye kazi hiyo.
Baada ya kutua na kujaza mafuta Tripoli , Libya, ndege hiyo iliendelea hadi Uganda na kutua Entebbe.

Wakati huo Idd Amin alishakorofishana na maswahiba wake Waisrael na kutangaza kuunga mkono harakati za
Wapalestina kuikomboa nchi yao. Kuna wakati, Idd Amin alishawahi
kutamka, kuwa anawaandaa askari wake kwenda kushiriki mapambano ya kuwandoa Wayahudi kwenye milima ya Golan waliyoiteka toka kwa
Wapalestina. Na Idd Amin alishaviamrisha vikosi vyake kufanya mazoezi ya kivita kujiandaa na operesheni ya kuikomboa milima ya Golan.
Naam, ndege ilipotua Entebbe, abiria wote walikaribishwa na Idd Amin mwenyewe. Siku mbili baadae, watekaji nyara walianza kutoa madai yao; walidai mateka wangeachiwa huru kama idadi kubwa ya wafuasi wa vikundi kadhaa vya kigaidi wangeachiwa huru kutoka kwenye magereza ya Ulaya na hata Afrika.

Ni katika tukio hili la utekaji nyara ndege ambapo kwa kiasi fulani
mateka walihisi kuwepo kwa tumaini la kukombolewa. Ni kwa vile
maofisa wengi wa jeshi la Israel wamefanya kazi Uganda ikiwemo kutoa
mafunzo ya kijeshi. Na kama kuna watu duniani waliokuwa wakimjua vema Idd Amin ikiwemo uwezo wa jeshi lake, basi, watu hao ni Waisrael.
Maofisa wengi katika jeshi la Idd Amin walipata mafunzo yao ya
kijeshi Israel.

Kabla ya operesheni hiyo iliyopewa jina la Thunderbolt kuanza, Mossad, Shirika la Ujasusi la Israel, liliamua kumtumia Jenerali wake mstaafu aliyeitwa Chaim Bal Lev. Bwana huyu alikuwa ni rafiki mkubwa na wa siku nyingi wa Jenerali Idd Amin. Wawili hawa walifanya mazungumzo ya muda mrefu na ya kirafiki kwa kutumia simu. Waliongea karibu siku zote kabla ya mateka kuokolewa.

Kwa kumtumia Jenerali huyu rafiki wa Amin, Waisrael walikuwa wanaiba muda ili kujiandaa zaidi, na vile vile kujaribu kumshawishi Amin asiwadhuru mateka hao na pengine kuwaachia huru.
Hata kama majasusi ya Kiyahudi walikuwa na michoro yote ya uwanja wa Entebbe ambao waliuchora wenyewe na kuujenga, lakini, kazi ya vikosi vya Israel kutua Entebbe haikuwa rahisi sana.
Hawakuwa na hakika ya ukubwa wa vikosi vya Amin uwanjani hapo.
Walitegemea zaidi , ufahamu wao wa uwanja wa ndege wa Entebbe. Maana, ni Waisrael waliojenga uwanja huo. Kutoka Tel- Aviv hadi Entebbe ni
mwendo wa takribani saa nne kwa ndege.

Uganda na Israel wamekuwa na mahusiano mazuri ya muda mrefu.
Mahusiano hayo yangalipo hadi hii leo. Ni kutokana na sababu za kihistoria.
Kabla ya Jumuiya ya Kimataifa kupendekeza makazi ya Wayahudi waliokuwa wametapakaa dunia nzima yawe katika Israel ya sasa, nchi ya Wapalestina, kulikuwepo na wazo la Wayahudi kutafutiwa makazi mapya katika nchi ya Uganda. Mpaka miaka ya karibuni, nchi pekee ya Kiafrika ambapo raia wa Israel hakuhitaji kuomba viza ni Uganda. Raia wa Uganda pia
hawakuhitaji pia kuomba viza ya kuingia Israel.

Tukirudi kwenye tukio lile la utekaji ndege. Kwa haraka, Waisrael
waliendesha operesheni ambayo si rahisi kusadikika. Makomandoo wa Israel waliruka kwa ndege kubwa kutoka Tel-Aviv kuelekea Entebbe.
Ndege yao ilitua saa sita na dakika moja usiku kwenye pembe ya mbali ya Uwanja wa Entebbe. Taa za ndani na nje ya dege lile kubwa zilizimwa wakati ndege ilipoukaribia uwanja wa Entebbe ikiwa na mwungurumo dhaifu. Mwungurumo usiosikika kwa mbali.

Waisarel walikuja na ndege mbili, moja ilibaki Nairobi ikiwa na
vifaa vya tiba na vingine muhimu. Iliyotua Entebbe ilibeba gari mbili,
Landrover na Mercedes Benz nyeusi.
Gari hizo zilitumiwa na makomandoo wa Kiyahudi kufika kwenye jengo walilokuwamo mateka. Waliwakuta mateka wote na wateka nyara wakiwa katika ukumbi wa mapunziko kwa abiria.
Amri ilitolewa kwa lugha ya Ki-hebrenia ikiwataka Wayahudi wote
wajilaze chini mara moja. Wote waliobaki wamesimama au kuinama kwa kusitasita, hawakupata sekunde zaidi za kutafakari. Risasi za
makomandoo wale ziliwamiminikia miilini mwao.
Operesheni ya kikomandoo iliyochukua takribani dakika tisini
pale Entebbe iliwaacha watekaji nyara saba bila uhai. Idadi ya askari wa Amin takribani ishirini nao waliuawa pale Entebbe. Mateka wote
walikombolewa isipokuwa mama wa miaka 75 Dora Bloch aliyekuwa
hospitalini Mulago, Kampala.

Inasemekana, kuwa mateka huyo akaja kuuawa na Idd Amin mwenyewe.Habari hiyo haijathibitishwa .

Kwa upande wao, Makomandoo wale wa Kiisrael walimpoteza Kanali Yoni Netanyahu. Komandoo yule aliuawa kwa kupigwa risasi ya usoni na askari mmoja wa Idd Amin. Miaka ishirini baadae, kaka wa Yoni Netanyahu akaja kuwa Waziri Mkuu wa Israel na ambaye ni Waziri Mkuu wa Israel wa sasa, jina lake ni Benjamin Netanyahu, ambaye leo ametua Entebbe Airport.
Huu ni Uchambuzi Endelevu

Post a Comment

0 Comments